MSAFARA wa wachezaji, benchi la ufundi pamoja na viongozi wa klabu ya Simba umewasili salama Kinshasa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo leo tarehe 10 Februari 2021, kwa ajili ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya AS Vita Club. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezo huo wa kwanza wa kundi A, utachezwa siku ya Ijumaa tarehe 12 Februari majira ya saa 1 usiku kwenye Uwanja wa Stade des Martyrs.
Simba iliondoka jana nchini kupitia Uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere majira ya saa 10 jioni ikiwa na msafara wa watu 44, kuelekea Ethiopia na leo asubuhi majira ya saa 10 asubuhi iliunganisha ndege na kuelekea Kinshasa, DR Congo.
Ikumbukwe mara ya mwisho kwa Simba kukutana na AS Vita Club kwenye uwanja huo ilikuwa msimu wa 2018/19 na kupoteza mchezo huo kwa mabao 5-0, licha ya kufanikiwa kufuzu kwenye hatua ya robo fainali.
Wachezaji pekee walioachwa kwenye msafara huo ni nahodha wao John Bocco ambaye anasumbuliwa na majeruhi pamoja na kiungo mshambuliaji wao Perfect Chikwende ambaye kanuni za mashindano hayo hazimruhusu kucheza mara baada ya uhamisho wake kutoka FC Platinum ya Zimbabwe.
Leave a comment