UONGOZI wa klabu ya Simba umeamua kushusha viingilio kutoka Sh. 3,000 mpaka Sh. 2,000, kwenye mchezo wao dhidi ya TP Mazembe kutoka Congo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezo huo ambao utakuwa wa mwisho kwenye michuano ya Simba Super Cup, utachezwa siku ya Jumapili tarehe 31 Januari 2021, kwenye Uwanja wa Benjamini Mkapa jijini Dar es Salaam majira ya saa 10 jioni.
Hayo yamethibitishwa na Afisa habari wa klabu hiyo, Haji Manara mara baada ya kumalizika kwa mchezo kati ya Simba dhidi ya Al Hilal ambao waliibuka na ushindi wa mabao 4-1.
“Mchezo wetu dhidi ya TP Mazembe tumeamua kushusha kiingilio kutoka Sh. 3,000 hadi Sh. 2,000 na tunaomba wanasimba wajitokeze kwa wingi,” alisema Manara.
Wakati akisema hayo tayari klabu ya TP Mazembe wameshawasili nchini leo mchana kwa ajili ya michuano hiyo ambayo inatumiwa na klabu hizo kujiweka sawa kuelekea hatua ya makundi ya Ligi ya mabingwa Afrika itakayoanza tarehe 12 Februari 2021.
Leave a comment