MIAMBA ya soka ya jijini Dar es Salaam nchini Tanzania ya Simba na Yanga inashuka dimbani katika michuano na muda tofauti leo Jumapili, tarehe 10 Aprili 2022. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Vinara wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2022/223, Yanga wao watahamishia makali yao kwenye Kombe la Azam Sports Federations Cup (ASFC) hatua ya robo fainali ikiwakaribisha Geita Gold Sports, Uwanja wa Benjamin Mkapa kuanzia saa 10:00 usiku.
Ikiwa Yanga itaibuka na ushindi, itamsubiri mshindi kati ya robo fainali nyingine itakayozikutanisha Simba dhidi ya Pamba FC utakaochezwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, tarehe itakayotangazwa baadaye.
Ni baada ya mchezo huo kusogezwa mbele kutoka 13 Aprili 2022 ili kuipisha Simba kufanya maandalizi ya mchezo wake wa robo fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Orlando Pirates utakaopigwa tarehe 17 Aprili 2022, Uwanja wa Mkapa.
Katika mchezo mwingine wa mapema leo Jumapili ni wa Simba dhidi ya Polisi Tanzania katika Uwanja wa Ushirika Mkoa wa Kilimanjaro ukiwa ni mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Simba inashika nafasi ya pili ikiwa na pointi 40 na mchezo mmoja mkononi itakaoucheza leo huku Yanga ikiwa kileleni na pointi 51 baada ya kushuka dimbani mara 19.
Ikiwa Simba ataibuka na ushindi leo, atakuwa amepunguza pengo la pointi na watani zake la pointi nane huku Azam FC ikishika nafasi ya tatu ikiwa na pointi 28 kati ya michezo 19 iliyokwisha kucheza.
Leave a comment