KLABU ya Simba, imefanikiwa kunyakuwa winga wa kimataifa wa Malawi, Duncan Nyoni ambaye amejiunga rasmi na kikosi hiko, kwa ajili ya msimu mpya wa mashindano. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezaji huyo ambaye anacheza nafasi ya winga, pamoja na mshambuliaji ametambulishwa hii leo na huenda akaja kuchukua nafasi ya Luis Miquissone aliyetimkia Al Ahly.
Simba inafanya usajili huo, huku kikosi chao kikiwa jijini Rabat nchini Morocco kwenye maandalizi kwa ajili ya msimu ujao wa mashindano.
Duncan mwenye umri wa miaka 23, amejiunga na Simba akitokea kwenye klabu ya Silver Strikers ya nchini Malawi kama mchezaji huru.
Simba inafanya usajili huo huku tayari ikiwa imeondokewa na wachezaji wake wawili ambao ni Miquisone pamoja na kiungo wake, Clatous Chama aliyetimkia kwenye klabu ya RS Berkane.
Miquissone amejiunga Al Ahly kwa ada ya uhamisho ya shilingi 2.3 bilioni, ambayo klabu ya Al Ahly imetoa kwenda Simba.
Kwa upande wa Chama tayari ameshajiunga na na club ya RS Berkane ya nchini Morocco kwa mkataba wa miaka mitatu.
Chama amesaini mkataba huo unaotajwa kuwa umeigharimu RS Berkane ada ya uhamisho ya Tsh Bilioni 1.5 kwenda Simba SC na kuongezewa mshahara mara nne ya aliokuwa analipwa Simba SC.
Chama ambae ameonekana kwenye mazoezi ya RS Berkane akiwa na Tuisila Kisinda wa Yanga, alijiunga na Simba SC mwaka 2018 akitokea Lusaka Dynamos ya Zambia.
Leave a comment