PENALTI ya dakika 60 ya mchezo iliwekwa kambani na Chriss Mugalu ilitosha kuipatia Simba pointi tatu kwenye mchezo wa ugenini dhidi ya AS Vita Club ya nchini DR Congo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mchezo huo wa kwanza wa kundi A, wa michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika ulishuhudia Simba akilipa kisasi kwa kuifunga AS Vita wakiwa kwao ambapo mara ya mwisho kukutana Simba alipoteza kwa mabao 5-0.
Simba ilianza mchezo huo huku ikichukua tahadhari ya kujilinda zaidi katika eneo lao la ulinzi na kufanya mashambulizi ya kushtukiza kutokana na ubora waliokuwa nao AS Vita, nakufanya timu hizo kwenda mapumziko bila bao.
Kipindi cha pili kilianza kwa Simba kuendelea kujihami zaidi huku wakiendelea kushambulia kwa kushtukiza na hatimaye kufanikiwa kupata penalti baada ya beki wa AS Vita kunawa mpira kwenye eneo la hatari.
Mugalu akiwa kwenye ardhi ya nyumbani alifanikiwa kupachika mpira huo kambani na kuipatia timu hiyo pointi tatu.
Kwa matokeo hayo Simba anakuwa kileleni kwenye msimamo wa kundi A, akisubiri mchezo unaofuata dhidi ya Al Ahly utakaochezwa Dar es Salaam, tarehe 23 Februari 2021.
Leave a comment