MABIGWA watetezi wa Kombe la Shirikisho Azam Federation CUP (ASFC), Simba ya Dar es Salaam, imetinga robo fainali ya michuano hiyo, baada ya kuibuka na ushindi wa 2-1 dhidi ya Kagera sugar. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Simba imeibuka na ushindi huo leo Jumamosi, tarehe 1 Mei 2021, katika mchezo huo, uliochezwa Uwanja wa Benjamin Mkapa, mkoani Dar es Salaam.
Kagera ilikuwa ya kwanza kujipatia goli, dakika ya 45, kupitia kwa Erick Mwijage akiunganisha pasi kwa kichwa ya Dickson Muhilu.
Timu hizo, zilikwenda mapumziko kwa Kagera ikiongoza 1-0.
Dakika 45 za kipindi cha pili, zilianza kwa kushuhudia, Kocha wa Simba, Didier Gomez, akimtoa kiungo mkabaji, Thadeo Lwanga na kumwingiza, Bernard Morrison, ambapo aliifanya Simba kuanza kulishambulia kwa kasi lango la Kagera.
Simba iliwachukua dakika kumi tangu kuanza kwa kipindi cha pili, ambapo Morrison aliisawazishia timu yake dakika ya 55 kwa kuunganisha pasi ya Louis Miquissone.
Dakika ya 67, Meddie Kagera aliifungia Simba goli la pili na la ushindi, akiunganisha pasi safi ya Morrison.
Leave a comment