KIKOSI cha Simba, viongozi pamoja na benchi la ufundi wamesafiri leo saa 4:30 na shirika la ndege la Air Tanzania kuelekea nchini Zimbabwe kwa ajili ya mchezo wa Klabu Bingwa Afrika dhidi Platinum FC ya nchini humo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Simba wanacheza mchezo huo wa mzunguko wa kwanza mara baada ya kufanikiwa kuwaondosha mabingwa wa Ligi Kuu nchini Nigeria, Plateau United kwenye hatua ya awali mara baada ya kuibuka na ushindi wa bao1-0 kwa michezo yote miwili.
Mchezo huo wa mzungo wa kwanza utachezwa tarehe 23 Disemba, 2020, kwenye uwanja wa Mandava uliopo jijini Harare, huku mchezo wa marudiano utapigwa tarehe 5 Januari, 2021 jijini Dar es Salaam kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa.
Kama Simba itavuka kwenye hatua hii kwa kuwaondosha Platinum itakuwa imefanikiwa kuingia kwenye hatua ya makundi ya michuano hiyo kama walivyofanya kwenye msimu wa 2018/19 na kama ikiondoshwa kwenye hatua hii, itadondokea kwenye Kombe la Shirikisho.
FC Platinum ni timu anayochezea mtanzania Elias Maguli ilifanikiwa kuvuka hatua hiyo mara baada kuwaondosha mabingwa wa Msumbuji Costa Do Sol kwa jumla ya mabao 4-1, kwenye michezo yote miwili.
Mara ya mwisho Platinum kucheza na timu kutoka Tanzania ilikuwa ni mwaka 2015, kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho dhidi ya Yanga ambapo ilipigwa mabao 5-2, katika michezo yote miwili.
Leave a comment