KLABU ya Simba kupitia kamati ya uchaguzi imetangaza rasmi mchakato wa uchaguzi mdogo wa klabu hiyo wa kujaza nafasi ya Mwenyekiti iliyoachawa wazi na Swedy Nkwabi mara baada ya kujiuzulu ndani ya klabu hiyo katika uchaguzi utakaofanyika tarehe 7 februari 2021. Anaripoti Kelvin Mwaipungu… (endelea)
Ilichukua mizei 10 kwa Nkwabi kuhudumu katika nafasi hiyo kama Mwenyekiti kabla ya tarehe 5 Novemba 2019 alipoamua kung’atuka mara baada kuandika barua kwenye bodi ya wakurugenzi ya kabu hiyo huku sababu kuwa ikiwa ni kuhitaji muda zaidi wa kushughulikia biashara zake binafsi.
Mara baada ya kujiuzulu kwa Nkwabi, bodi ya wakurugenzi kupitia kwa wenyekiti wake Mohammed Dewji ilimteuwa Muhina Seif Kaduguda ambaye alidumu kwenye nafasi hiyo kama kaimu kwa muda wa mwaka moja na mwezi mmoja.
Akizungumza mbele ya waandishi wa habari leo tarehe 13 Disemba 2020 kwenye Hotel ya Serena jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa kamati hiyo Boniface Lihamwike alisema kuwa wamedhamiria kufanya uchaguzi wa huru na haki ili wanasimba wapate nafasi ya kumchagua mtu wamtakaye.
“Nawaahidi huu utakuwa uchaguzi huru na haki, mtu yoyote atakayetaka kuomba nafasi hiyo basi tutatengeneza mazingira yenye usawa ili wanasimba waweze kupata kiongozi wanaomtaka kwa kufuata kanuni” alisema Boniface Lihamwike.
Mchakato huo wa uchaguzi utaanza kuanzia tarehe 14-21 Disemba 2020 kwa wanachama wote wenye sifa kwenda kuchukua fomu kwenye Makao Makuu ya klabu hiyo mtaa wa Msimbazi jijini Dar es Salaam, kwa gharama ya shilingi 300,000 na zoezi la kurudisha fomu litafungwa tarehe 24 Disemba 2020, majira ya saa 10 jioni.
Pia Kamati hiyo imeleza kuwa tarehe 29 Disemba 2020, itatangaza majina ya waliopitishwa kuwania nafasi hiyo na kisha kutoa muda wa kupokea mapingamizi na tarehe 2 januari 2021, kamati hiyo itapitia mapingamizi hayo.
Uchaguzi huo utatoa fursa kwa wanachama wa klabu ya Simba kumchagua kiongozi huyo atakaye kwenda kuwawakilisha kwenye bodi ya wakurugenzi wa klabu hiyo.
Kamati hiyo ilisitiza kuwa vigezo vya kuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo ni lazima uwe na kadi ya uwanachama kwa kipindi cha miaka mitatu na elimu kuanzia shahada ya kwanza inayotambulika na tume ya vyuo vikuu nchini (TCU)
Leave a comment