KLABU ya Simba leo imeingia mkataba wa kiasi cha Sh. bilioni mbili na kampuni ya Vunja Bei Group, ambapo watakuwa watengenezaji na wasambazaji wa jezi pamoja na vifaa mbalimbali kupitia nembo ya klabu hiyo. Anaripoti kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mkataba huo umesainiwa leo tarehe 20 Aprili, 2021 jijini Dar es Salaam, ambapo kwa upande wa Simba uliwakilishwa na Mtendaji Mkuu wa klabu ya Simba, Barbara Gonzalez huku kwa upande wa kampuni ya Vunja Bei Group iliwakilishwa na Mkurugenzi wake, Fred Fabian.
Katika hafla hiyo iliyofanyika Mlimani City Dar es Salaam, Mtendaji Mkuu wa klabu hiyo, Gonzalez alisema wakati wa mchakato wa kutafuta kampuni hiyo ya kufanya kazi walipokea maombi kutoka makampuni mbalimbali ndani na nje ya nchi na kuamua kufanya kazi na Vunja Bei mara baada ya kukizi vigezo.
“Katika mchakato tulipokea maombi kutoka makampuni mbalimbali kwa ajili ya kutengeneza na kusambaza jezi za Simba, lakini mara baada ya kuchanganua tukaamua kufanya kazi na kampuni ya Vunja Bei ambayo leo naitangaza rasmi kama washindi wa zabuni hii,” alisema Barbara.
Aidha mtendaji huyo, alisema kuwa thamani ya mkataba huo ni shilingi bilioni 2 na kuweka historia ya timu ya kwanza kwenye ukanda wa Afrika Mashariki kusaini mkataba mkubwa kama huo kwenye upande wa usambazaji na utengenezaji wa jezi.
Kwa upande wa Vunja Bei Group, Fabian alisema kuwa haikuwa kazi ndogo kwa kampuni changu kama wao kupata nafasi ya kuaminiwa na kupewa tenda kama hii kutokana na ushindani ulivyokuwa wakati wa mchakato huo.
“Tunashukuru klabu ya Simba kwa kutupa nafasi na kuzingatia uweledi kwenye mchakato huu, haikuwa rahisi kutokana na makampuni makubwa waliotaka hii tenda, lakini tulijiamini mimi na timu yangu na tumeweza kufanikisha hili,” alisema Fred.
Mkataba kati ya pande mbili hizo utaanza msimu ujao wa Ligi kwa kutengeneza jezi na vitu mbalimbali vyenye nembo ya klabu ya Simba kuanzia timu za vijana (wanawake na wanaume) mpaka timu ya wakubwa.
Mapema mwaka huu Simba, ilitangaza mchakato wa kutafuta mzabuni kwa ajili ya kazi ya hiyo ya kutengeneza na kusambaza jezi kuanzia msimu ujao wa Ligi mara baada ya mkataba uliopo sasa na kampuni ya Uhuru Sports kufikia ukingoni.
Leave a comment