WATANI wa jadi nchini Tanzania, Simba na Yanga, watakutana kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, tarehe 3 Julai 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ni baada ya mchezo kuahirishwa kuchezwa Jumamosi iliyopita ya yarehe 8 Mei 2021, katika Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.
Mchezo huo uliokuwa uchezwe uwanjani hapo kuanzia saa 11:00 jioni, haukufanyika baada ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), kuusogeza hadi saa 1:00 usiku.
TFF ilisema, ilisogeza mbele mchezo huo, baada ya kupokea maelekezo kutoka serikalini.
Uamuzi wa kusogezwa mbele, ulitolewa mchana wa siku hiyo, hali iliyowafanya Yanga kugomea mabadiliko hayo na kusisitiza mchezo huo uchezwe muda uleule wa saa 11:00 jioni.
Yanga ilisema, mabadiliko hayo ni kinyume cha kanuni namba 10(15) cha ligi kuu, kinachotaka mabadiliko hayo kutolewa saa 24 kabla ya siku ya mchezo.
Baada ya kuahirishwa na suala hilo kutua bungeni, Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa aliagiza wizara ya habari, utamaduni, saana na michezo kukaa na TFF na vilabu husika kulimaliza suala hilo.
Waziri wa wizara hiyo, Innocent Bashungwa alikutana na TFF na viongozi wa timu hizo na bodi ya ligi na kukubaliana mchezo huo utapangiwa siku ya kuchezwa.
Leo Jumapili, tarehe 16 Mei 2021, Bodi ya Ligi Kuu, imetoa ratiba ya ligi hiyo huku ikionyesha, mchezo huo utapigwa 3 Julai 2021, Uwanja wa Benjamin Mkapa, Dar es Salaam, kuanzia saa 11:00 jioni.
Leave a comment