SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF), limeagiza mechi kati ya Simba SC na Al-Merrikh ya Sudani, inayotarajiwa kufanyika tarehe 16 Machi 2021 katika Uwanja wa Benjamini Mkapa, jijini Dar es Salaam, kufanyika bila mashabiki uwanjani. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Ofisa Habari wa Klabu ya Simba, Haji Manara, leo Jumamosi tarehe 13 Machi 2021, wakati akizungumza na wanahabari, jijini Dar es Salaam.
Simba na Al-Merrikh wanatarajiwa kukutana kwenye mechi hiyo ya marudio ya Kombe Klabu Bingwa barani Afrika. Mechi ya awali iliyochezwa Sudani, hawakufugana.
Manara amesema, taarifa hiyo ya CAF kuhusu zuio la mashabiki wa Simba kuingia uwanjani, ni agizo la Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).
“Wakati tukijiandaa na mechi hii, tulipoke taarifa kupitia TFF ambayo ilitoka CAF, ikituagiza au ikituamuru mechi yetu ya tarehe 16 Machi 2021, ichezwe bila mashabiki,” amesema Manara.
Manara amesema, zuio hilo limetokana na janga la mlipuko wa corona, ambapo CAF imechukua hatua hiyo kudhibiti maambukizi mapya ya virusi hivyo.
“Hakuna sababau nyingine yoyote zaidi ya kuchukua tahadhari dhidi ya corona, ndio maana kama mnakumbuka mechi iliyopita waandishi pia mlitakiwa mpimwe kabla ya kuingia kwenye mechi,” amesema Manara.
Licha ya pigo hilo, Manara amesema Simba Sc itatumia uzoefu wake wa kucheza bila ya sapoti ya mashabiki uwanjani, kushinda mechi hiyo, ili kupata alama tatu zitazowaweka katika mazingira mazuri ya kutinga robo fainali ya michuano hiyo.
“Tulipata sare ugenini bila mashabiki na tunakuja nyumbani bila mashabiki, tutashinda. Wachezaji watumie uzoefu huo wa kucheza bila mashabiki kuushinda mchezo huo,” amesema Manara.
Afisa habari huyo amesema, kama klabu hiyo ikiondoka na alama tatu katika mechi hiyo, itabaki na kibarua cha kusaka alama moja katika mechi mbili ilizobakiza katika kundi A.
Simba Sc imebakisha mechi mbili ngumu, ambapo itashuka dimbani kuchuana na Klabu ya Vita na Al Ahly.
Leave a comment