LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara 2020/21, inaendelea leo Jumatano tarehe 10 Machi 2021, ikizikutanisha Simba na Tanzania Prisons, katika Uwanja wa Benjamin Mpaka, mkoani Dar es Salaam. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Timu hizo, zitashuka kwenye dimba hilo kuanzia saa 1:00 usiku.
Prisons inashuka kuwakabili mabingwa hao watetezi, wakiwa na kumbukumbu wa ushindi wa goli 1-0, katika mchezo wa mzunguko wa kwanza, uliochezwa tarehe 22 Oktoba 2020, Uwanja wa Nelson Mandela- Sumbawanga, mkoani Rukwa.
Prisons, wanaojinasibu kwa kucheza mpira ‘gwaride’ walikuwa timu ya kwanza, kuwafunga Simba ambayo siku nne baadaye yaani tarehe 26 Oktoba 2020, ikakubali kipigo kingine cha 1-0, kutoka kwa vijana wa kupapasa, Ruvu Shooting.
Ruvu waliipiga Simba, katika mchezo uliochezwa Uwanja wa Uhuru, mkoani Dar es Salaam.
Ni timu mbili pekee za Prisons na Ruvu ambazo mpaka sasa ndizo zimeifunga Simba, ambayo inashika nafasi ya pili ya msimamo ikiwa na pointi 45, baada ya kushuka dimbani mara 19 huku vinara wa ligi hiyo, Yanga ina pointi 50, baada ya kucheza michezo 23.
Utakuwa mchezo wa ama, Prisons waendeleze ubabe wao au Simba walipe kisasi.
Simba, imetumia mitandao yake ya kijamii kuzungumzia mchezo huo ikisema “mnyama tunaenda kuwakabili askari magereza. Mechi ya kulipa kisasi.”
Ikiwa Simba itashinda, itafikisha alama 48 na michezo mitatu mkononi na kuchagiza mbio za kutetea ubingwa huo na iwapo, Prisons wataifunga Simba, watafikisha pointi 30 na kuwafikisha nafasi ya nane ya msimamo.
Leave a comment