BODI ya Ligi Tanzania Bara imetoa ratiba ya michezo iliyohairishwa kwenye mzunguko wa kwanza wa Ligi, ambapo klabu ya Simba itaanza kushuka dimbani tarehe 4 Februari 2021 itakapo wakabili Dodoma Jiji FC. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Ligi hiyo inataanza tarehe 13 Februari 2021, kwa michezo ya raundi ya 19 mara baada ya kumpuzika kupisha michuano ya kombe la mapinduzi na michuano ya Kombe la Mataifa Afrika kwa wachezaji wa ndani.
Simba ambayo ilikuwa na mechi tatu mkononi itaanza kuikabili Dodoma Jiji siku hiyo katika mchezo utakaopigwa kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma majira ya saa 10 jioni.
Mara baada ya mchezo huo Simba itashuka tena dimbani tarehe 7 Februari 2021, ambapo itawaalika Azam FC kwenye mchezo utakaofanyika kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.
Michezo mingine ambayo itapigwa kukamilisha viporo hivyo ni Kmc dhidi ya Namungo FC utakaochezwa 4 Februari 2021, na Namungo dhidi ya Ruvu Shooting mchezo utakaopigwa tarehe 7 Februari 2021 kwenye Uwanja wa Majaliwa Lindi.
Aidha Bodi hiyo imesema kuwa michezo mingine kati ya Namungo dhidi ya Gwambina na Namungo dhidi ya Simba itapangiwa tarehe nyingine.
Michezo hiyo iliahirishwa kutokana na klabu za Simba na Namungo kushiriki michuano ya Ligi ya mabingwa na Kombe la Shirikisho barani Afrika.
Leave a comment