FATMA Karume, wakili na aliyekuwa Rais wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), amesema siku 100 za uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, zilikuwa ngumu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Akizungumza na MwanaHALISI Online kuhusu siku 100 za Rais Samia madarakani amesema, rais huyo alipokea madaraka wakati taifa likiwa vipande. Rais Samia anatimiza siku 100 madarakani Jumapili, tarehe 27 Juni 2021.
Hata hivyo amesema, Rais Samia amejitahidi kufanya vizuri katika suala la haki za binadamau, ingawa hatua yake ya kumteua aliyekuwa Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), Biswalo Mganga, kuwa Jaji wa Mahakama Kuu, imemtia doa.
“Jengine alilofanya Rais Samia katika siku 100, ni suala la haki za watu. Amesimamia lakini ametuangusha kumchukua Biswalo Mganga kuwa Jaji.
“Ameniangusha sababu hakustahili kuwa jaji kwani kwa miaka mitano akiwa DPP, kadhulumu haki zao, hafai kuwa jaji lakini kahakikisha kamuweka,” amesema Fatma.
Sehemu nyingine ambayo Rais Samia ameanza vizuri ni kuipa uhuru Ofisi ya Mkazuzi Mkuu wa Serikali (CAG), na kwamba kwa sasa inatekeleza majukumu yake bila woga.
Rais Samia aliingia madarakani tarehe 19 Machi 2021, kufuatia kifo cha mtangulizi wake, Hayati John Magufuli, kilichotokea katika Hospitali ya Mzena mkoani Dar es Salaam, tarehe 17 Machi 2021.
Fatma amesema, Rais Samia alipokea nchi wakati ilikuwa katika mchakato wa bajeti ya mwaka wa fedha wa 2021/2022 huku akitakiwa kukamilisha safu yake ya uongozi, katika kipindi hicho, kazi ambayo aliimudu vizuri.
“Kwenye siku 100 za Rais Samia, kwa kizungu it was busy hundred days (zilizuwa siku 100 ngumu). Kwanza kaipata nchi katika wakati mgumu, ikiwa inaingia kwenye mchakato wa bajeti 2021/2022.
“Wakati wa CAG (Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali), anatoa ripoti yake, kwa hivyo alikuwa na mambo ashughulikie, yakae sawa ili aweze kuendesha nchi,” ameeleza Fatma.
Amesema, katika kipindi hicho Rais Samia alikuwa na jukumu la kupokea kijiti cha Uenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kutafuta makamu wake wa rais, pamoja na kuunda baraza la mawaziri, jambo ambalo pia amelimudu.
“Kulikuwa na mchakato wa uenyekiti wa CCM, aliumudu. Kulikua na mchakato atafute makamu wake, kaumaliza. Ilibidi atizame cabinet yake, kuna wengine hatupendi watu aliowarejesha kwenye baraza lakini ilibidi afanye hiyo kazi na kaifanya,” amesema Fatma.
Rais Samia alimteua aliyekuwa Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Phillip Mpango, kuwa makamu wake wa Rais.
Mwanaharakati huyo amesema, sehemu nyingine ambayo Rais Samia aliimudu katika siku 100, ni kushughulikia janga la ugonjwa wa homa kali ya mapafu, inayosababisha na Virusi vya Corona (Covid-19).
Hata hivyo, Fatma kasema baadhi ya wasaidizi wake aliowarithi katika uongozi uliopita, wanamkwamisha katika mapambano dhidi ya ugonjwa huo.
“Alipoingia ilibidi atizame suala la Covid-19, kalisimamia na anakwenda nalo vizuri. Anafuata ushauri wa watalaamu na ukumbuke kwamba Serikali aliyoirithi, amerithi na mawaziri wake, hawataki ushauri wa watalaamu. Walikuwa wanapiga nyungu, kwa hivyo uwanja hauko sawa na bado tunaona hawako naye,” amesema Fatma.
Fatma ameongeza “tunaona makamu wa rais havai barakoa, lakini yeye alivyoshika nchi alituambia tuvae barakoa, hajawahi kutoka hata mara moja bila barakoa.”
Fatma amesema, sehemu nyingine aliyofanya vizuri Rais Samia, ni kukataa dhulma pamoja na kurudisha mahusiano ya kidiplomasia.
“Alisisitiza kwamba Serikali yake haitaki dhulma, kamueleza vizuri CAG kwamba hataki uongo anataka ukweli na CAG kasema ukweli. Kabadilisha mfumo wake wa mambo ya nje,”
“Katika siku hizi siku 100, kaenda Kenya, Uganda na Maputo nchini Msumbiji. Anazungumza katika mikutano ya kikanda, kajaribu kurejesha diplomasia yetu, ilikuwa imedorora,” amesema Fatma.
She is doing very well, she will leave a good legacy if she can deliver a new constitution and a new independent election commission like the South African or Kenyan one.