RAIS Samia Suluhu Hassan, amesema haridhishwi na kasi ya utendaji wa bandari za Tanzania na kuwataka watendaji waache siasa na longolongo wakati wa utekelezaji majukumu yao. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo akizungumza katika hafla ya utiaji saini mkataba wa ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR), iliyofanyika leo Jumatatu, tarehe 4 Julai 2022, jijini Dar es Salaam.
“Siridhishwi kabisa na kasi za bandari, siasa na longolongo zilizopo, huko nje mabandari yanaendeshwa kwa kasi kubwa, yanaendeshwa kwa operesheni na biashara zinaenda kwa kasi zaidi. Mwekezaji anakuja ni kuzungushwa mwanzo mwisho. Bandari wafanye kazi tutatupia jicho vizuri kwenye masuala ya bandari wale waliokabidhiwa bandari nataka tuelewane vizuri,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema, kama Bandari ya Dar es Salaam, ingekuwa inafanya kazi vizuri, mapato yake yangegharamia nusu ya bajeti ya Serikali kila mwaka.
“Bandari hii ikifanya kazi vizuri nusu ya bajeti tunayopanga kila mwaka, itatolewa bandari ya Dar es Salaam, lakini tu kama tutajipanga tufanye kazi vizuri kama bado tunakwenda kwa longolongo hilo lengo hatutafikia, nawaomba wajiange vizuri tujenge kwa kasi,” amesema Rais Samia.
Leave a comment