KATIKA jitihada za kuunga mkono serikali ya awamu ya sita katika utoaji wa elimu, Shule Kimataifa ya Hazina ya Magomeni jijini Dar es Salaam imeanza kutoa elimu ya awali bure. Anaripoti Mwandishi Wetu….(endelea)
Elimu hiyo ya bure inatolewa kwa muda wa miezi mitatu kuanzia Oktoba, Nobemba hadi Desemba kwa wanafunzi wa shule ya awali kuanzia chekechea yaani baby class, Middle Class na Pre Unit.
Mkuu wa shule hiyo, Juma Omar alisema watakachochangia wazazi wa wanafunzi hao ni chakula na sare za shule pekee ila hawatatozwa ada.
Akizungumza kwa nini shule hiyo imeamua kutoa elimu hiyo bure, mwalimu Omar alisema wameamua kurejesha sehemu ya faida kwa jamii kwa kuwaamini kwa miaka mingi.
Alisema wazazi wameiamini shule hiyo kwa muda mrefu na kuwapa wanafunzi kila mwaka hivyo wameaona watoe zawadi ya elimu hiyo bure kama motisha kwao.
“Tungependa wazazi waje waone tunafanya nini hadi tunaongoza wilaya ya Ilala na wakati mwingine Mkoa wa Dar es Salaam kwenye mitihani ya kitaifa,” alisema
Aidha, alisema baadhi ya wazazi wameanza kuitikia wito huo na kuanza kupeleka watoto wao na kwamba shule hiyo itaakauwa na uwezo hata wakupokea wanafunzi zaidi ya 100 kama watajitokeza.
“Hazina inawashukuru wazazi ambao wametuamini kwa muda mrefu na tunawaomba waendelee kutuamini kwa kutuletea watoto wao na wachangamkie fursa hii ya masomo bure hadi Desemba,” alisema
Aliahidi kuwa shule hiyo itaendelea kufanya vizuri kwenye matokeo ya mitihani ya kitaifa kutokana na mazingira mazuri ya kusomea na ari ya ufundishaji ya walimu wa shule hiyo.
Mmoja wa wazazi, Halima Hussein, alisema yeye kama mzazi amefurahishwa na hatua hiyo ya Hazina kwani inawapa moyo wazazi na itawasaidia wale wasio na uwezo kupeleka watoto wao.
“Hii ni mara ya kwanza kusikia shule ya kimataifa na bora kama Hazina inatoa ofa ya aina hii kwa hiyo nawashauri wenzangu wachangamkie fursa hii kwa kuwaandikisha watoto wao wanufaike na elimu bure,” alisema Halima
Minza Mulele kwa upande wake alisema kwa shule hiyo kuamua kutoa elimu bure kwa miezi mitatu ni jambo la kupongezwa na linalopaswa kuigwa na shule zingine.
“Shule zisiangalie faida tu kila wakati zinapaswa kutoa huduma wakati mwingine ndiyo maana nawapongeza sana Hazina kwa uamuzi huu wa kutoa elimu bure kwa miezi mitatu,” alisema Mulele.
Leave a comment