KESI inayotarajiwa kuwa mashuhuri na ya aina yake kati ya Tundu Lissu, aliyevuliwa ubunge wa Jimbo la Singida Mashariki dhidi ya Job Ndugai, Spika wa Bunge, sasa kuunguruma. Anaripoti Bupe Mwakiteleko … (endelea).
Kesi hiyo inatarajiwa kuanza leo tarehe 15 Agosti 2019, katika Mahakama Kuu, Kanda ya Dar es Salaam Lissu akipinga uamuzi wa Spika Ndugai kumvua ubunge.
Lissu, mmoja wanasheria mashuhuri nchini, alifungua shauri la kupinga kuvuliwa ubunge wake, kwenye mahakama hiyo Jumatano, tarehe 7 Agosti 2019, chini ya hati ya dharura.
“Maombi ya kesi hii yatasikilizwa mbele ya Jaji Mtupa. Hati ya wito wa mahakama inabainisha kuwa mlalamikiwa ambaye ni Spika Ndugai, atatakiwa kufika mahakamani bila kukosa,”
imeeleza taarifa ya Tumaini Makene, Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya Chadema na kuongeza;
“Tunatoa wito kwa viongozi, wanachama, wafuasi wa Chadema na Watanzania wote wapenda haki, demokrasia na utawala bora unaoheshimu sheria, mahali popote walipo kufuatilia kwa karibu mwenendo wa shauri hilo kuanzia hatua ya sasa.”
Spika Ndugai alitangaza uamuzi wa kumvua ubunge Lissu, tarehe 28 Juni 2019, wakati akiahirisha mkutano wa 15 wa Bunge. Hatua hiyo iliibua sintofahamu na kupingwa.
Kiongozi huyo wa Bunge, alitaja sababu za kumvua ubunge Lissu kuwa: Kushindwa kuhudhuria vikao vya bunge bila kutoa taarifa kwa maandishi kwa spika na kutojaza fomu ya taarifa za mali na madeni kwa mujibu wa sheria ya maadili ya viongozi wa umma ya mwaka 1985.
Lissu kupitia kaka yake, Alute Mughwai, anaomba Mahakama Kuu imruhusu kufungua shauri la kupinga kuvuliwa ubunge wake, kupitia utaratibu wa Judicial Review – mapitio ya maamuzi yaliyofikiwa.
Lakini pia Lissu anaiomba mahakama itoe amri ya muda ya kusimamisha kuapishwa kwa mbunge mteule wa jimbo la Singida Mashariki (CCM), Miraji Mtaturu.
Lissu anaiomba mahakama isikilize na kutoa uamuzi wa maombi yake haraka, vinginevyo Mtaturu ataapishwa kushika wadhifa huo, na kwamba, hatua yoyote ya kutosikiliza shauri lake kwa haraka, litamuathiri moja kwa moja kwa kuwa amepoteza haki zake zote.
Leave a comment