JOHN Shibuda, Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Siasa Tanzania, amesema Rais John Pombe Magufuli, aliumizwa na sintofahamu iliyojitokeza katika uchaguzi wa serikali za mitaa wa tarehe 24 Novemba 2019. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Shibuda amesema hayo leo Ijumaa tarehe 17 Julai 2020 wakati akizungumza katika warsha ya wadau wa uchaguzi katika kujadili namna ya kudhibiti rushwa kwenye Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020 iliyoandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) iliyofanyika jijini Dar es Salaam.
Katika uchaguzi huo wa serikali za mitaa, vyama zaidi ya vitani vya upinzani Chadema, CUF, ACT-Wazalendo, NCCR-Mageuzi, UPDP, Chaumma na CCK havikushiriki kwa kile kilichoelezwa kutokutendewa haki kwa wagombea wao hasa nyakati za kuchukua au kurejesha fomu za kuomba kuteuliwa kugombea.
Soma zaidi hapa
Kujitoa huko, kulikifanya chama tawala Chama Cha Mapinduzi (CCM) kushika kwa zaidi ya asilimia 98 uchaguzi huo.
Akizungumzia sakata hilo, Shibuda amesema Rais Magufuli alimshirikisha masikitiko yake juu ya dosari zilizojitoleza kwenye uchaguzi huo na Waziri wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Seleman Jafo alishindwa kutengua matokeo hayo.
“Niwaeleze, Rais Magufuli aliumia sana na hizo kasoro zilizokuwa nje ya utendaji wake. Na Jaffo alikuwa hana kanuni za kutengua yale yaliyokuwa na hila,” amesema Shibuda
“Nasema hilo sababu mimi alinishirikisha na aliniambia hapa natoka vipi?. Nawaambia Rais hakufurahia na kasoro zilizojitokeza,” amesema Shibuda.
Kufuatia dosari hizo, Shibuda ametoa wito kwa mamlaka husika kuhakikisha uchaguzi mkuu unakuwa huru ili dosari hizo zisijitokeze.
“Ndio maana nasema uchaguzi huu uwe wa haki usawa ili wengine waone Tanzania ni nchi kimbilio na darasa la siasa za demokrasia,” amesema Shibuda ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Chama cha ADA-Tadea
Leave a comment