PETER Madeleka, Wakili wa Mahakama Kuu ya Tanzania na mtetezi wa haki za binadamu, amedai sheria ya uhujumu uchumi inatumika kama nyundo kwa wanyonge. Anaripoti Jemima Samwel, DMC … (endelea).
Ametoa kaulihiyo tarehe 11 Mei 2021, alipokutana na waandishi wa habari katika Hoteli ya Selena, Dar se salaam ambapo amesema, sheria za makosa ya jinai zinajulikana lakini amedai serikali inafanya tofauti na sheria zinavyoelekeza.
Wakili huyo amesema, sheria ya uhujumi uchumi kwa miaka ya hivi karibuni, imekuwa ikitumika vibaya, kwa baadhi ya makosa ya uhujumi uchumi ambayo hayana dhamana.
Na kwamba, sheria hiyo imekuwa ikitumika kama nyundo ya kuwapiga na kuwaumiza wanyonge, ambao kwa bahati mbaya hawana uelewa wa kutosha kuhusu sheria hiyo.
“Sheria ya uhujumi uchumi ni sura ya 200 kwa sheria za Tanzania, lakini kosa la uhujumi uchumi kwa sasa utakaa gerezani hata zaidi ya mwaka mmoja kwa kisingizio kwamba, upelelezi haujakamilika. Jambo hilo ni kinyume cha sheria.
“Kifungu kidogo cha kwanza cha sheria ya uhujumi uchumi kinasema, pamoja na mambo mengine, ili upelelezi wa uhujumi uchumi uweze kufanyika, lazima uwepo na amri ya kufanya uchunguzi huo au upelelezi huo.
“Amri hiyo itangazwe kwenye gazeti la serikali, sharti hilo ni sharti la lazima, lisipotekelezwa au lisipozingatiwa, maana yake ni kwamba sheria nzima na mwenendo wake unakuwa ni batili,” amesema Madeleka.
Amesema, kuna mashtaka mahakamani ambayo upelelezi haujakamilika ama upelelezi haukamiliki kutokana na kutofuata sheria.
“Uendeshaji wa kesi za uhujumi uchumi hauzingatia kifungu cha sheria cha 21 (1) ambacho kinasema, lazima gazeti la serikali litangaze amri ambayo inatoa ruksa ya upelelezi huo.
“Kosa la pili ambalo linafanyika kuhusiana na kosa la uhujumi uchumi, lipo chini ya kifungu cha 25 (1) cha sheria ya uhujumi uchumi, ieleweke kwamba sio kila wakili wa serikali anayeendesha kesi hizi, anaruhusiwa,” amesema.
Wakili Madeleka amesema, wakiri wa serikali wa kuendesha mashtaka ya uhujumi uchumi, ni lazima awe ametangazwa kwenye gazeti la serikali.
“….lakini udhoefu unaonesha, mawakili wanaenda kuendesha kesi mahakamani bila kuwa na uthibitisho wa uhalali wa kuendesha kesi hiyo. Jambo hilo sio sahihi huku mahabusu wanaendelea kusota magereza bila kufata sheria,” amesema Madeleka.
Leave a comment