KATIBU wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam nchini, Sheikh Ponda Issa Ponda, ameishauri Serikali iweke misingi imara itakayosaidia kujenga uhuru wa kudumu wa sekta ya habari kutekeleza shughuli zake bila vikwazo. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Sheikh Ponda ametoa ushauri huo leo tarehe 16 Januari 2023, akizungumza na wanahabari kuhusu mchakato wa marekebisho ya sheria zinazosimamia sekta ya habari, unaofanywa na Serikali kwa kushirikiana na wadau.
“Nashauri viongozi kuhakikisha wanaweka misingi imara ili tasnia iepukane na hali ya sheria ambazo zinapunguza uwezo wao wa kufanya kazi kama sheria kandamizi ambazo zimejitokeza huko nyuma. Aweke misingi imara kuhakikisha anmgalau sekta ya habari inapumua kutokana na mazingira yaliyojitokeza kwenye maeneo mengi,” amesema Sheikh Ponda.
Akizungumzia manufaa ya vyombo vya habari kuwa huru, Sheikh Ponda amesema itasaidia kuaminika kwa umma kwa kuwa vitawasilisha taarifa kwa usahihi, pamoja na ksuaidia Serikali na sekta binafsi kutathimini shughuli zao za kila siku.
“Uhuru wa vyombo vya habari faida yake ya kwanza ni malengo ya kuanzishwa chombo cha habari yatakuwa yamefikiwa kwa sababu bila shaka chombo cha habari kinatakiwa kiwe huru. Lakini pia vikiwa huru vitaaminika kwa umma maana yake vitaeleza au vitawasilisha zile fikra za umma kwa usahihi kwa maana hiyo chombo kitaaminika kwa umma,” amesema Sheikh Ponda.
Kiongozi huyo wa dini amesema “yale matakwa ya wananchi au ukosoaji yatafikiwa, lakini vikiwa huru vitasaidia kusambaza elimu inayohitajika katika jamii. Vitasaidia mataifa ya nje kufahamu hadhi ya taifa lao, uchumi wao na hali ya kisiasa ikoje kiasi kwamba watu wa mataifa mengine watajipanga kuleta ushirikiano mzuri sababu watakuwa wanafahamu vizuri ile hali ya taifa.”
Aidha, Sheikh Ponda amesema demokrasia ikiimarika itasaidia kuimarisha utendaji wa vyombo vya habari.
“Ikiwa kuna demokrasia vyombo vya habari vitakuwa hai, maana yake sheria zitakuwa nzuri sio zile za ukandamizaji sababu kinyume na demokrasia ni udikteta yaani mabavu, kwamba watu hawapati uhuru wa kuzungumza, kukosoa na kadhalika,” amesema Sheikh Ponda.
Leave a comment