TAASISI na Jumuiya za Kislamu Tanzania imemuomba Spika wa Bunge Job Ndugai nakala ya mahojiano ya Kamati ya Maadili, Haki na Madaraka ya Bunge. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Akizungumza na Mwandishi wa Habari hizi, Sheikh Issa Ponda Katibu wa Taasisi na Jumuiya hizo amesema taasisi hiyo imeomba nakala hiyo ili kubaini ukweli juu ya uamuzi wa Spika Ndugai wa kutaka Bunge kutofanya kazi na Profesa Mussa Assad, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.
Sheikh Ponda amesema kuwa upo mkanganyiko kati ya uamuzi wa Bunge uliosomwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Emmanuel Mwakasaka na majibu ya Profesa Assad kwa vyombo vya habari.
“Kwa kuwa suala hili ni zito na lina pasua jamii na hata kuwagawa wananchi na Wabunge wao, ni muhimu likawa wazi zaidi ili wananchi walifahamu katika uhalisia. Kwa sababu hiyo sisi kama viongozi wenye fursa na ukaribu mkubwa na Jamii tunaomba tupatiwe nakala halisi (Hansard) ya mazungumzo kati ya Kamati ya Maadili, Haki na Madaraka ya Bunge lako na CAG ili tuelewe kwa usahihi mwenendo wa shauri na kusaidia kulifikisha kwa umma kama lilivyokuwa,” amesema Sheikh Ponda.
Amesema kuwa kwa kusema Bunge dhaifu haiwezi kuwa sababu ya kuamua kutofanya kazi na CAG; “Upo ukweli uliojificha hapa ndio maana tunaomba rekodi za maandishi na video za mahojiano ya Profesa Assad na Kamati ya Maadili.”
Leave a comment