SHEIKH wa Mkoa wa Dodoma, Alhaji Mustafa Rajabu amekemea vikali vitendo vya kikatili na unyanyasaji ambavyo vinafanywa na baadhi ya watu na kueleza kuwa vitendo hivyo ni kinyume na makusudi ya Mwenyezi Mungu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Sheikh Rajabu ametoa onyo hilo leo tarehe 8 Julai mwaka huu wakati wa ibada ya Ijumaa iliyofanyika katika Msikiti wa Gaddafi Jijini Dodoma.
Kiongozi huyo wa kiroho amesema kwa sasa yamejitokeza matendo maovu ya ukatili na unyanyasaji jambo ambalo halikubaliki machoni pa Mwenyezi Mungu na jamii kwa ujumla.
Akitoa mawaidha msikitini hapo Sheikh Rajabu amesema katika kipindi hiki cha mwezi mtukufu na kuelekea sikukuu ya kuchinja ni wajibu wa kila muumini wa dini ya kiislamu kuhakikisha wanatenda matendo yaliyomema ikiwa ni pamoja na kuwasaidia wale wasiojiweza.
“Tunahitaji kuwa na watu ambao ni wacha Mungu ambao wanakuwa na hofu ya Ki-mungu kwa maana hiyo jamii inatakiwa kuchukia matendo maovu yakiwemo ya unyanyasaji pamoja na kuwaonea walio wanyonge.
“Tumeshuhudia baadhi ya watu wakifanya unyanyasaji wa kijinsia kwa kusababisha mauji na wakati mwingine kusababisha manyanyaso kwa watoto wadogo na wengine kuwafanyia matendo maovu.
“Naiasa jamii kuachana na matendo maovu ya kikatili na badala yake tunatakiwa kuhakikisha tunakuwa wacha Mungu kwa kipindi chote kwa kutenda matendo mema yanayompendeza Mungu” ameeleza Sheikh Rajabu.
Aidha, katika mawaidha hiyo pia ameambatana na maombi maalumu ya kuliombea Taifa pamoja na kumuombea Rais Samia Suluhu Hassani.
Maombo hayo pia yalikuwa maalumu katika kuliombea Baraza la Mawaziri pamoja na viongozi wa serikali ili wafanye kazi kwa kutenda haki kwa kila mmoja.
Leave a comment