ALHAD Mussa Salum, Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam amesema, Kama Sheikh Aboubakar Zuberi, Mufti Mkuu wa Tanzania angemruhusu kujiunga na chama cha siasa, angejiunga na Chama cha NCCR-Mageuzi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Sheikh Alhad ametoa kauli hiyo leo Ijumaa tarehe 7 Agosti 2020, katika Mkutano Mkuu wa chama hicho unaofanyika katika Ukumbi na Diamond Jubilee, Dar es Salaam.
“Kama Mufti Mkuu angeruhusu, ningeomba kadi ya NCCR – Mageuzi lakini Mufti haruhusu kuingia kwenye siasa, chama hichi kimeonesha kinapambana kwa siasa safi, lugha nzuri na ya staha bila kufikiria umwagaji wa damu na uvunjifu wa Amani, tunataka siasa ya aina hii,” amesema Sheikh Salum.
Amesema, Tanzania inapaswa kuongozwa na watu wenye uchungu na sio wale wanaotumika na mabeberu.
“Nchi hii lazima iongozwe na wenye uchungu na wazalendo hatutakubali kuongozwa na watu ambao wanatumika na mabeberu. Hiki kitu hakitawezekana, lazima iongozwe na wazalendo, moja kati ya wazalendo hao ni Mheshimiwa Mbatia,” amesema Sheikh Mussa.
Kiongozi huyo wa Waislamu mkoani Dar es Salaam amewataka viongozi wa vyama vya siasa kuendesha siasa safi, kwa ajili ya kuwapa afya Watanzania.
“Siasa safi inawapa afya Watanzania, si siasa za kupinga kila kitu. Tunataka siasa zenye jicho la sawasawa palipo nyooka unasema pamenyooka tena kwa lugha nzuri na namna nzuri, huu ni ukomavu wa kisiasa ambao Mwenyekiti Mbatia ameounyesha kwa Watanzania,” alisema Sheikh Alhad.
Mchungaji Lewis Hiza kutoka Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), amevitaka vyama vya siasa kushirikiana ili kuijenga Tanzania.
“Mimi ni mfuatiliaji sana wa viongozi mbalimbali wa vyama, niseme toka moyoni kwamba, kama kuna kitu nafurahi nikimsikiliza mwenyekiti wenu (Mbatia) neno Tanzania huwa analipa nguvu ya pekee, hupenda kusema Mama Tanzania.
“Niseme tu kwamba, tunawatakiwa mshikamano na Mungu aliruhusu katika nchi yetu tuwe na vyama mbalimbali na kusudi tushirikiane vipaji katika kuijenga nchi, kuwahudumia Watanzania,” amesema Mchungaji Hiza.
Sheikh Mussa Kundecha, aliyekuwa Amiri wa Shura ya Maimamu nchini Tanzania amewataka wanasiasa kutumia hekima katika shughuli zao.
“Mimi kama Kundecha ni muumini wa falsafa na hekima, kuna msemo wa kiarabu unasema, kueleza jambo kwa kitendo ni fasaha zaidi kwa kueleza, kuliko kusema kwa maneno,” amesema Kundecha.
Dk. Camilius Kassala, Mwakilishi wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), amevitaka vyama vya siasa kuiga mfano wa NCCR-Mageuzi kutumia busara katika kutafuta suluhu ya changamoto wanazokabiliana nazo.
“Kama mfumo wa vyama vingi kama demokrasia, vyama vingi vya siasa vinatupa shida hapa na pale kuhusu hili na lile, ni kwa sababu ya jambo moja ambalo NCCR-Mageuzi mnajitahidi sana kulizingatia na suala hilo nimekuwa nikilisema hapa na pale mara nyingi,” amesema Dk. Kassala.
Leave a comment