MAHAKAMA Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, maarufu Mahakama ya Mafisadi, imewahukumu kifungo cha maisha gerezani, mfanyabiashara, Abdul Nsembo na mkewe Shamim Mwasha baada ya kukutwa na hatia ya makosa ya kujihusisha na biashara ya dawa za kulevya aina ya Heroin. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Pia, mahakama hiyo ya mafisadi, imetoa amri ya kutaifisha mali zao ikiwemo gari aina ya Discover 4 na iwe mali ya Serikali na kuagiza hizo kuteketezwa.
Hukumu ya kesi, imetolewa leo Jumatano tarehe 31 Machi 2021, na Jaji Elinaza Luvanda baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili kati ya Jamhuri na utetezi na kujiridhisha watuhumiwa wamekutwa na hatia katika makosa mawili ya usafirishaji dawa za kulevya.
Shamimu anayemiliki Blog ya 8020 na mumewe,walikuwa wanakabiliwa na mashtaka ya kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroini gramu 439, tukio wanalodaiwa kulitenda tarehe 1 Mei 2019, eneo la Mbezi Beach mkoani Dar es Salaam.
Wawili hao, walikutwa na kesi ya kujibu Septemba mwaka 2020 na kutakiwa kujitetea mahakamani hapo.
Ni baada ya ushahidi wa mashahidi sita na vielelezo nane, vilivyokuwa vimetolewa na upande wa mashtaka.
Wanandoa hao, kwa mara ya kwanza walifikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam tarehe 13 Mei 2019, wakikabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi.
Leave a comment