KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) wa Chama Cha Mapinduzi( CCM), Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka ameiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii, kupeleka mara moja tochi maalumu za kusaidia kufukuza tembo kwa vikundi vilivyoundwa ili kukabiliana na wanyama hao wilayani Meatu, Mkoa wa Simiyu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Simiyu … (endelea).
Shaka ameyasema hayo leo Jumanne tarehe 1 Februari 2022, kwa nyakati tofauti akiwa wilayani Meatu, alipokuwa katika ziara ya kukagua uhai wa chama mashinani ikiwa ni sehemu ya ziara ya Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa inayoongozwa na Katibu Mkuu wa CCM, Daniel Chongolo mkoani humo.
Amesema ulinzi wa wananchi dhidi ya wanyama wakali na waharibifu ni jukumu muhimu ambalo linapaswa kupewa kipaumbele na kwamba hatua ya wananchi kujitolea kushirikiana na mamlaka zinazohusika kuzuia wanyama hao zinapaswa kuungwa mkono.
“Nitazungumza na Wizara ya Maliasili na Utalii leo walete tochi zinaohitajika. Nimeambiwa kuna vikundi vya wananchi vimeundwa na vinahitaji tochi hizo kwa ajili ya kusaidia kufukuza tembo wanaoingia katika makazi ya watu. Wizara ilete haraka tochi hizo,” amesema.
Amesema maelekezo ya CCM kwa kuzingatia Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020-2025 Ibara ya 69 vifungu vidogo vya (b) na (c), Chama kinaitaka Wizara ya Maliasili na Utalii iweke mikakati thabiti ya kuwalinda wananchi dhidi ya wanyamapori kupitia vifaa maalumu vya kuwafukuza au kuwazuia wasifike katika maeneo ya makazi.
Shaka amesema Ilani inaielekeza wizara hiyo kuwajengea uwezo wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi kupitia vikundi ili wawe na uwezo wa kuwafukuza wanyamapori wanapovamia maeneo yao bila kuleta madhara.
“Hatuwezi kuutukuza uhifadhi unaowaumiza wananchi wetu na kuwapa umaskini huku kukiwa hakuna hatua stahiki zinazochukuliwa. Hali hii ikiachwa hivi, wananchi watachoka na wataanza kuwadhuru wanyamapori tulionao wakiwemo tembo wanaovamia kwenye mashamba na makazi ya wananchi na kuleta madhara,” amesema
Awali, katika risala ya wazee wa wilaya hiyo walipokutana na Shaka, iliyosomwa na Mzee Emmanuel Masanga, wamempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanyia ikiwamo kuweka historia ya kuwawezesha wanafunzi wote waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza kuanza masomo kwa pamoja.
Mzee Emmanuel amesema wazee wa wilaya hiyo wanaiona kwa macho kazi kubwa inayofanywa na Rais Samia na kwamba wataendelea kumuunga mkono huku wakihamasisha vijana kuchapa kazi kwa bidii ili kujiletea maendeleo.
Leave a comment