KESI inayomkabili Mbunge wa Kawe, Halima Mdee katika Mahakama Hakimu Mkazi Kisutu, ya kutoa lugha chafu dhidi ya Rais John Magufuli imekwama kusikilizwa leo tarehe 8 Oktoba 2018 baada ya shahidi upande wa mashtaka kushindwa kufika mahakamani. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Katika kesi hiyo, mashahidi upande wa mashtaka walitakiwa kutoa ushahidi wao, lakini hawakufika kitendo kilichosababisha upande wa mashataka kukosa shahidi na kesi hiyo kuahirishwa.
Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba alipanga tarehe 22 Oktoba 2018 kesi hiyo kuendelea kusikilizwa baada ya Wakili Mwandamizi wa Serikali, Patrick Mwita kudai kwamba shahidi waliyemtarajia kufika mahakamani hapo leo, yuko nje ya mkoa wa Dar es Salaam.
Licha ya kuiahirisha kesi hiyo, Hakimu Simba amesema kesi hiyo ifikapo mwezi Desemba mwaka huu iwe imeisha.
Mashahidi watatu akiwemo Mrakibu wa Polisi (SP) Batseba Kasanga Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Urafiki upande wa mashtaka tayari wameshatoa ushahidi kuhusu kesi hiyo.
Mdee anadaiwa mnamo tarehe 3 Julai 2017 akiwa katika makao makuu ya Chadema Kinondoni jijini Dar es Salaam alitoa lugha chafu dhidi ya rais Magufuli.
Katika kesi hiyo, inadaiwa kuwa Julai 3, 2017 katika Makao Makuu ya Ofisi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) iliyopo mtaa wa Ufipa wilaya ya Kinondoni, Mdee anadaiwa kutamka maneno dhidi ya Rais John Magufuli kuwa “anaongea hovyo hovyo , anatakiwa afungwe breki.”
Kauli hiyo inadaiwa kwamba ingeweza kusababisha uvunjifu wa amani.
Leave a comment