SERIKALI ya Tanzania, imesema itatumia Sh. 6.0 bilioni, kwa ajili ya ujenzi wa nyumba 20 za viongozi, katika makao makuu ya nchi, jijini Dodoma. Anaripoti Jemima Samwel, DMC…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatatu, tarehe 31 Mei 2021, bungeni jijini Dodoma na Naibu Waziri Ujenzi na Uchukuzi, Mwita Waitara, akimjibu Mbunge Viti Maalum (CCM), Mariam Ditopile Mzuzuri.
Katika swali lake, Mzuzuri alihoji “je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za viongozi waandamizi wa Serikali, kama makatibu wakuu na mawaziri katika Mji wa Dodoma, kwa ajili ya makazi ya viongozi hao?”
Akijibu swali hilo, Waitara amesema fedha za ujenzi wa nyumba hizo, zimetengwa katika mwaka wa fedha wa 2020/2021, na kwamba hatua za ubunifu na usanifu wa ujenzi, zimekamilika.
“Hivi sasa kwa kutumia Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), hatua za ubunifu na usanifu wa nyumba hizo pamoja na makadirio ya gharama za ujenzi zimekamilika. Aidha, ukarabati wa nyumba za viongozi jijini Dodoma unaendelea,” amesema Waitara.
Aidha, Waitara amesema, katika mwaka huo wa fedha, Serikali imetenga Sh. 4 bilioni, kwa ajili ya ukarabati wa nyumba 40 za viongozi jijini humo.
“Pamoja na ujenzi wa nyumba hizi, Serikali pia imetenga fedha kwa ajili ya kuendelea na ukarabati wa nyumba nyingine 40, za Viongozi zilizopo jijini Dodoma, katika maeneo ya Kisasa, Area D na Kilimani,” amesema Waitara.
Ni utumiaji mbaya wa fedha za wananchi