WAZIRI wa Afya, Ummy Mwalimu, amekiri kuwepo kwa changamoto za utoaji wa huduma za afya katika mkoa wa Njombe ikiwemo suala la upungufu wa majengo ya kutolea huduma na vifaa tiba vya kisasa vya kurahisisha huduma ya afya. Anaripoti Felister Mwaipeta, TUDARCo … (endelea).
Waziri Ummy ameeleza hayo leo Jumanne tarehe 9 Agosti, 2022, wakati wa uzinduzi wa jengo la mama na mtoto katika Hospitali Rufaa Mkoa wa Njombe.
Kutokana na hali hiyo Waziri Ummy amesema Sh 10.7 bilioni zimetolewa na Serikali ya awamu ya sita katika kukamilisha ujenzi wa mradi huo wa kisasa ambapo una zaidi ya wodi 200 pamoja na vitanda 200 ambavyo vitakuwa toshelevu kwa wananchi wa mkoa wa Njombe.
Pia amesema Hospitali hiyo itapatiwa vifaa vya kisasa kama CT scan ili wananchi kupata huduma hiyo pasipo kwenda hospitali za mbali.
Katika ziara hiyom Waziri Ummy aligusia suala la umuhimu wa wananchi wote hususani wa mkoa wa Njombe kutumia bima ya afya ili kuepuka gharama za matibabu wanapo hitaji huduma za afya kwenye vituo vya kutolea huduma za afya.
Katika hatua nyingine Waziri Ummy amewasihi wananchi wote kushiriki kikamilifu katika zoezi la sensa ya watu na makazi ili kuwezesha Serikali kupamga bajeti toshelevu kwa wananchi wote.
Leave a comment