MFANYABIASHARA bilionea na Mwenyekiti Mtendaji wa Kampuni ya PAP, Habinder Seth amesalimu amri kwa Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP). Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Seth amemwandikia DPP Dk. Biswalo Mganga barua ya kukiri mashitaka ya uhujumu uchumi, kufuatia mashtaka 12 yanayomkabili katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam.
Wakili Michael Ngalo, anayemuwakilisha Seth mahakamani hapo, leo tarehe 10 Oktoba 2019 amesema mteja wake amemuandikia barua DPP kukiri makosa yake pamoja na kuomba msamaha.
Wakili Ngalo ameeleza hayo mbele ya Huruma Shahidi, Hakimu Mkazi Mkuu, wakati kesi inayomkabili Seth na mwenzake, ilipokuja kutajwa.
Wankyo Simon, Wakili wa Serikali ameieleza mahakama hiyo kwamba wamepokea barua ya mtuhumiwa huyo, wanaifanyia kazi, na kisha watatoa majibu.
Miongoni mwa mashtaka yanayomkabili Seth pamoja na James Rugemalira, Mkurugenzi wa Kampuni ya VIP, ni utakatishaji fedha na kusababisha hasara ya Sh. 309 bilioni (Dola za Marekani 22,198,54.60), kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu, kujihusisha na mtandao wa uhalifu na kutoa nyaraka za kughushi.
Leave a comment