NAIBU Waziri wa Habari, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza amesema, Shirikisho la Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFA) haliwezi kupokea moja kwa moja fedha za misaada kutoka Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA) kwa kuwa, sio mwanachama wa shirikisho hilo. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Shonza ametoa kauli hiyo leo tarehe 7 Februari 2019 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu maswali ya Hatib Said Haji, aliyehoji namna ZFA inavyonufaika na fedha za FIFA.
Katika maswali yake, Haji alitaka kujua ZFA inapataje fedha kutoka FIFA huku akidai kuwa, ZFA imekuwa ikikosa fedha hizo kwa kuwa, kuna mkanganyiko kuhusu masuala ya muungano huku Zanzibar kiwa na wizara yake ya michezo pamoja na shirikisho lake wakati Tanzania Bara ikiwa na wizara na shirikisho lake la mpira wa miguu (TFF).
“Kiasi gani cha mgao wa FIFA waliwahi kuipatia Zanzibar, mmewahi kuipatia mgawo wowote Zanzibar kutoka fedha za FIFA, kwa sababu TFF siyo chombo cha muungano, waziri na wizara ya michezo sio ya muungano.
“Anaposema msaada unaokuja mgao utaenda ZFA, nataka kujua zitaenda vipi ikiwa Zanzibar wana wizara yao, kuna mkanganyiko ndio maana tunakosa msaada wa FIFA,” amehoji Haji.
Akijibu maswali hayo, Shonza ameeleza kuwa, ZFA haiwezi kupokea fedha za misaada kutoka FIFA moja kwa moja kwa kuwa siyo mwanachama wa shirikilo hilo na sio mwanachama wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani Afrika (CAF) bali ZFA inapokea fedha hizo kutoka kwa TFF.
“Suala la michezo sio la muungano, ni kwamba ZFA ni sehemu ya TFF kwa tafsiri hii fedha zinazotolewa hugawanywa, ZFA si mwanachama wa CAF na si mwanachama wa FIFA bali iko ndani ya TFF. Kwa maana yake itapata fedha kutoka TFF,” amesema Shonza.
Kuhusu kiasi cha fedha za FIFA ambazo ZFA imepokea kutoka kwa TFF, Shonza amesema, TFF imekuwa ikitoa fedha kwa ZFA kwa ajili ya kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi na ukarabati wa uwanja wa Gombani.
Mnamo mwaka 2017, Zanzibar iliondolewa uanachama wa CAF ikiwa ilidumu katika uanachama huo kwa muda wa miezi mine tu.
Miongoni mwa sababu za Zanzibar kuporwa uanachama ni pamoja na kuwa sehemu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hivyo sheria za shirika hilo haziruhusu uanachama wa mashirikisho mawili kutoka kwa Taifa moja.
Leave a comment