SERIKALI imewaomba viongozi wa dini, waendelee kuelimisha wananchi kudumisha amani na umoja, ili kuleta maendeleo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Wito huo umetolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, leo tarehe 28 Septemba 2023, akizungumza katika Baraza la Maulid, jijini Dodoma.
Waziri Majaliwa amewataka viongozi wa dini kuiombea Serikali pamoja na nchi kwa ujumla, ili iendelee Kupata mafanikio.
“Niwasihi kuendelea kuliombea dua taifa letu tunatambua dua ni kitu muhimu Kwa ustawi wa Binadamu na jamii yetu, muendelee kuwaombea viongozi wetu, Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na Makamu wa Rais, Dk. Phillip Mpango, ili watuongoze Kwa busara, hekima na upendo katika kuliongoza Taifa letu,” amesema Waziri Majaliwa.
Katika hatua nyingine, Waziri Majaliwa amewaomba viongozi wa dini kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuwahamasisha wananchi kushiriki michakato ya uchaguzi, ikiwemo kujiandikisha katika daftari la majina ya wapiga kura na siku ya kupiga ya kura.
“Kabla ya uchaguzi mkuu hata huu ujao wa 2024, kutakuwa na zoezi la maborehso ya daftari la mpiga kura, Serikali inawategeme viongozi wa dini katika kuwahamasisha waumini kujitokeza kuhakiki majina Yao, baadae kushiriki katika kutoa elimu Kwa wananchi Wetu ili wajitokeze kupiga kura. Kauli yenu inasikilizwa Sana,” amesema Waziri Majaliwa.
Waziri Majakiwa amewataka viongozi wa dini kushirikiana na Serikali katika kutokomeza biashara ya dawa za kulevya kwa kuwa inaongezeka kwa kasi ulimwenguni huku matumizi yake yakiongezeka kuanzia mijini na vijijini, kitendo kinachomaliza nguvu kazi ya Taifa kwa kuharibu afya za vijana.
Pia, amewataka washiriki katika kampeni za kuhamasisha wananchi kutunza mazingira ili kukabiliana na athari zake ikiwemo mabadiliko ya tabia ya nchi na ukame.
Naye Waziri wa Viwanda na Biashara, amewataka viongozi wa dini kuhimiza Jamii kulinda amani na umoja ili kuleta maendeleo.
“Kwa ujumla tumehusiwa tushikamane katika kamba ya Mungu na Wala tusifarakiane, Mtume alituunganisha pamoja nasi hatuna zaidi ya kuungana katika kuyaendea yaliyomema na kukataa maovu. Tunapoadhimisha siku ya Leo tuhusiane mema, tushikamane na tuendelee kuliombea Taifa letu na viongozi wakiongozwa na Rais Samia,” amesema Dk. Kijaji.
Aidha, Dk. Kijaji amewataka viongozi wa dini,wazazi na walezi hasa kina mama, wawafundishe maadili watoto wao ili kujenga kizazi chema.
“Kauli mbiu tumeiona ni maulid, maadili na maendeleo kama dunia tumeiumba sana hivyo kwenye maadili ni muhimu sana bila maadili hatuwezi kufanikiwa,” amesema Dk. Kijaji.
Leave a comment