SERIKALI ya Tanzania, imeunda kikosi maalum kitachoshirikiana na wadau mbalimbali, kwa ajili ya kudhibiti wanyamapori wakali na wahalibifu katika maeneo yanayozunguka hifadhi. Anaripoti Nasra Bakari, DMC…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja, leo Jumatatu tarehe 10 Mei 2021, bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Dennis Londo, Mbunge wa Mikumi, Morogoro.
“Je, serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Wananchi wanaoishi kwenye vijiji vinavyopakana na hifadhi pamoja na mali zao, wanakuwa salama kwani wanyamapori wamekuwa wakiingia na kufanya uharibifu kwenye vijiji,” amehoji Londo.
Waziri Masanja amesema, serikali inatambua vijiji vinavyozunguka hifadhi za wanyamapori nchini, vinakabiliwa na changamoto ya wanyamapori wakali na waharibifu kama vile Tembo, Simba, Nyati, Viboko na Mamba.
Amesema, katika kupambana na wanyamapori hawa, serikali imeunda kikosi maalum cha kupambana nao, hususani kwenye maeneo yanayozunguka hifadhi kwa kadri taarifa za matukio zinavyopatikana.
“Aidha, serikali imeandaa mpango mkakati wa kitaifa wa kushughulikia wanyamapori wakali na wahalibifu, ambao unatoa mwongozo wa namna nzuri ya kuwawezesha wananchi kutumia maeneo yao bila kuathiriwa, mikakati hiyo ni pamoja na;-
Kutoa mafunzo kwa wananchi wanaoishi maeneo ya pembezoni mwa hifadhi kuhusu mbinu bora za kukabiliana na wanyamapori wakali na wahalibifu, mafunzo haya ni endelevu na yatafanyika katika maeneo yote yenye changamoto.
Pia kuimarisha vikosi vya doria za kudhibiti wanyamapori vikiwemo vitendea kazi ili viweze kufanya doria na kushirikiana na Halmashauri za wilaya na vijiji ili kuwezesha uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi.
Masanja amesema, Wananchi wa Mikumi na maeneo mengine yanaozunguka hifadhi, waendelee kutoa ushirikiano na
kufuata maelezo ya wataalam.
Leave a comment