SERIKALI ya Tanzania, imetoa utaratibu mpya wa kutoa maiti zinazodaiwa gharama za matibabu, hospitalini na kwamba kuanzia sasa kutakuwa na mfumo utakaowezesha ndugu kulipa taratibu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumanne, tarehe 6 Julai 2021 na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Dorothy Gwajima, alipotembelea Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), jijini Dar es Salaam.
Dk. Gwajima amesema, hatua hiyo ni utekelezaji wa agizo Rais Samia Suluhu Hassan, alilotoa hivi karibuni kwa wizara hiyo, kuhakikisha maiti zenye madeni hospitalini hazizuiwi, kwa ajili ya kutoa nafasi kwa ndugu zao kuzika.
“Wananchi wote mnaouguza tunawaombea ndugu zetu wapone warudi nyumbani, ikitoeka mapenzi ya Mungu yametimia ameitwa mbele ya haki, msiwe na wasiwasi hospitali zetu zinatekeleza agizo la Rais Samia, mwili utapatikana,” amesema Dk. Gwajima.
Dk. Gwajima ameongeza “kama una changamoto ya kulipia huduma, utaratibu wa kupewa bili yako kidogo kidogo umewekwa na utaboreshwa.”
Akielezea utaratibu huo unavyofanya kazi, Dk. Gwajima amesema ndugu wa wagonjwa watajaza fomu maalumu, kama wadhamini endapo lolote litatokea.
“ Wewe mwenye ndugu ukifika kuna utaratibu wa kujaza taarifa kwamba mimi ndio mdhamini wa mgonjwa na uatartibu huu hauzuii mgonjwa kuendelea kupata huduma kama wewe mdhamini hujafika,” amesema Dk. Gwajima.
Leave a comment