SERIKALI ya Tanzania, imewataka wananchi kuchukua tahadhari dhidi ya mlipuko wa ugonjwa Polio, ulioibuka hivi karibu katika nchi jirani ya Malawi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tahadhari hiyo imetolewa leo Jumamosi, tarehe 26 Februari 2022 na Mganga Mkuu wa Serikali, Dk. Aifello Sichalwe, ikiwa ni siku siku tisa tangu Malawi na Shirika la Afya Duniani Kanda ya Afrika (WHO), kuripoti mlipuko wa ugonjwa huo.
Kupitia taarifa hiyo, Dk. Sichalwe ametoa wito kwa wadau wa afya nchini kushirkiana katika jitihada za kupambana na magonjwa ya milipuko ikiwemo wa Polio.
“Wizara inaendelea kutoa wito kwa wadau katika ngazi zote, kuendelea kushirikiana kutekeleza jitihada mbalimbali za kupambana na magonjwa ya milipuko, ikiwemo ugonjwa huu kwa kuzingatia kikamilifu miongozo inayotolewa na wizara,” imesema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo imesema “ikiwa pamoja na kuwapeleka watoto kwenye vituo vya kutolea huduma za afya, ili wakakamilishe chanjo dhidi ya ugonjwa wa Polio.”
Wakati huo huo, taarifa ya Dk. Sichalwe imesema ugonjwa huo hauna tiba zaidi ya kinga, na kuitaka jamii kuhakikisha watoto wadogo hasa walio chini ya umri wa miaka mitano, wanakamilisha chanjo ya Polio, inayotolewa kwa awamu nne.
“Ni muhimu watoto wote walioko kwenye jamii zetu wawe wamekamilisha upataji wa chanjo hiyo, njia nyingine ambayo huweza kuzuia ugonjwa huu ni kutumia maji safi na salama, kuzingatia usafi wa mikono na mazingira,” imesema taarifa hiyo.
Taarifa hiyo imesema, virusi vya Polio huzaliana katika utumbo na huweza kuathiri mfumo wa fahamu, ikiwa pamoja na kupooza kwa ghafla kwa viungo ndani ya masaa machache na hata kupelekea kifo.
Taarifa ya Dk. Sichalwe imesema, Wizara ya Afya inaendelea kufanya tathimini ya hatari ya ugonjwa huo, kwenye mikoa inayopakana na nchi ya Malawi, Mbeya, Songwe na Ruvuma, ikiwa pamoja na kufuatilia wagonjwa wanaohisiwa kuwa na dalili za Polio, kupitia vituo vya afya.
Imesema Serikali itaendelea kuimarisha huduma ya chanjo ya Polio zinazotolewa kwa watoto wote nchini.
2