SERIKALI imesema kuwa jumla ya wananchi 367,985 wa halmashauri ya wilaya ya Tarime wanapata huduma za afya katika hospitali ya wilaya hiyo Tarime Mjini pamoja na vituo vya afya nane, huku vitano vikiwa vya serikali na vitatu vya binafsi na zahanati 23 huku 16 vikiwa vya serikali na saba za binafsi. Anaripoti Danson Kaijage, kutoka bungeni Jijini Dodoma … (endelea).
Kauli hiyo ilitolewa jana Bungeni na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais –TAMISEMI, Josephat Kandege alipokuwa akijibu swali la mbunge wa Tarime Vijijini John Heche (Chadema).
Mbunge huyo alitaka kujua ni kwanini serikali isipandishe hadhi hospitali ya wilaya ya Tarime na kuwa hospitali ya mkoa kutokana na hospitali hiyo kwa sasa kulemewa na wagonjwa wengi.
“Hospitali ya Wilaya ya Tarime imelemewa na mzigo wa wagonjwa kwa sababu inapokea wagonjwa wengi kutoka wilaya ya tarime na Rorya pamoja na uchache wa vituo vya afya katika maeneo mengi ya wilaya hiyo, Je ni kwanini serikali isipandishe hadi hospitali hiyo na kuwa hospitali ya mkoa,” alihoji Heche.
Kandehe katika majibu yake alisema kuwa ni kweli kuwa hospitali hiyo hinahudumia wilaya ya Tarime, Rorya, Musoma na Bunda na wagonjwa kutoka nchi jirani ya Kenya na kusababisha msongamano wa wagonjwa.
Hata hivyo alisema kuwa serikali haina mpango wa kupandisha hadhi hospitali hiyo kuwa hospitali ya Mkoa kwa kuwa mkoa wa Mara huna hospitali ya rufaa iliyopo Musoma Mjini.
“Ili kutatua changamoto za utoaji wa huduma za afya katika mkoa wa mara, serikali katika mwaka wa fedha 2018/19 imetenga kiasi cha Sh. 4.5 bilioni kwa ajili ya ujenzi wa hospitali tatu za halmashauri katika halmashauri ya za Bunda, Rorya na Musoma.
“Tayari fedha zote zimepelekwa kwenye halmashauri husika kwa ajili ya kuanza ujenzi, vile vile serikali inaendelea na ukarabati na ujenzi wa vituo sita vya afya katika mkoa wa Mara vinavyogharimu jumla ya Sh. 2.4 bilioni.
“Ujenzi wa hospitali tatu za halmashauri na vituo sita vya afya utaimarisha huduma katika ngazi ya msingi na kupunguza msongamano wa wagonjwa katika hospitali ya wilaya ya Tarime”alieleza Kandege.
Leave a comment