KAMPUNI ya Reli (TRL), imetangaza kubomoa nyumba zote zilizojengwa kando kando mwa reli inayotoka Dar es salaam, Moshi hadi jijini Arusha, anaandika Angela Willium.
Kadhalika, TRL imetangaza kuanza kuifanyia ukarabati mkubwa reli hiyo ili ianze kutumika kusafirishisha mizigo kama ilivyokuwa miaka ya nyuma.
Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam , Mkurugenzi wa TRL, Majanja Kadogosa katika ziara ya Naibu Waziri wa Ujenzi ,Uchukuzi na Mawasiliano, Atashasta Nditiye amesema baadhi ya nyumba zilizopo kwenye eneo la reli wameshaziwekea alama ya X.
Amesema alama ya X imeweka katika mikoa ya Morogoro na Dodoma ambapo inajengwa reli kubwa ambayo itapitisha Treni ya kutumia umeme.
“Tunawaomba wananchi waliovamia maeneo ya reli kuondoka mapema kabla ya kuanza zoezi la bomoa bomoa nyumba zao tumeshaziweka alama ya X”.
Kadogosa amesema wamekuwa na changamoto ya ubovu wa reli pamoja na upungufu wa wafanyakazi na kuomba waboreshewe maslai ya watumishi.
Kuhusu ujenzi wa reli ya mikoa ya Kaskazini, alisema wameshaanza na kwamba hivi sasa wamefika Mombo na itachukua miezi 7 hadi 8 kukamilika.
Kwa upande wake, Nditiye amesema kutokana na changamoto iliyopo ya kuwaondoa wananchi waliovamia eneo la reli aliwaomba kupisha na kwamba ambao wataingiliwa na reli watalipwa fidia.
Ukarababti wa reli ya Moshi hadi Arusha utakamilika ifikapo mwaka 2019 na lengo la ujenzi huo ni kukuza uchumi wa Tanzania na kutoa huduma kwa wananchi kwani gari moshi itabeba mizigo na nyingine itachukua abiria.
Leave a comment