SERIKALI imeondoa zuio la wafanyabiashara kuendeleza maeneo yao yaliyopakana na barabara ya Kimara Mwisho hadi kwa Kichwa, jijini Dar es Salaam. Anaripoti Hamis Mguta…(endelea).
Zuio hilo limeondolewa leo tarehe 12 Oktoba 2019 na Kisare Makori, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo wakati akizungumza na wananchi wa Kata ya Kimara na Saranga eneo la Darajani, Mtaa wa Mavurunza, Dar es Salaam.
Makori amechukua hatua hiyo, kufuatia malalamiko ya wafanyabiashara hao, kuzuiwa kuyaendeleza maeneo yao kwa madai ya kutorasimishwa pamoja na kwenye eneo la barabara.
“Naondoa zuio la kutokuendeleza maeneo yenu kwa kigezo kuwa yapo barabarani hadi pale hoja zenu za msingi zitakapotatuliwa,” ameeleza Makori.
Makori amewaagiza wamiliki wa maeneo hayo, kuyarasimisha ili kuondoa migogoro.
“Kwa wale ambao hawakufanyiwa Urasimishaji, kampuni iliyohusika itarudi kufanya shughuli hiyo. Kwa wamiliki wa maeneo yaliyopo kando ya barabara hiyo ya kutoka Kimara hadi kwa Kichwa,” amesema Makori.
Aidha, Makori amesema Serikali ikihitaji kuyatumia maeneo hayo, wananchi watapatiwa fidia kwa mujibu wa sheria na taratibu.
Fadhili Hussein, Afisa Mipango miji wa Manispaa ya Ubungo akitolewa ufafanuzi suala hilo, amesema kwa mujibu wa nyaraka, barabara ndio imewafuata wananchi, na kwamba wananchi hawakufuata barabara.
Hussein ameeleza kuwa, kwa mujibu wa sheria, kama Serikali itataka maeneo hayo kwa matumizi, wamiliki wake watapewa fidia.
Wakato huo huo, Makori ameeleza miradi ya maendeleo ambayo Wilaya ya Ubungo inatekeleza.
Makori amesema Wilaya ya Ubungo imetengewa kiasi cha Tsh. Bilioni 2.9, kwa ajili ya matengenezo ya barabara, ikiwemo barabara ya mtaa wa Mavurunza, ambao umetengewa Sh. 42 bilioni 42 ambazo zitakarabati maeneo korofi.
Aliwaagiza Wakala wa Barabara (Tanroad), Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (Tarura) na Mipango miji kuondoa changamoto zilizopo ndani ya siku saba.
“Tumepokea Tsh. Milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Kimara ambayo tunajenga ghorofa. Pia, Halmashauri imenunua eneo Kibesa ambalo lina thamani ya Tsh. Milioni 333 kwa ajili ya shughuli za kilimo na tayari imeshalipa Tsh. Milioni 150,” amesema Makori.
Kuhusiana na sekta ya maji, Makori amesema serikali imeingia mkataba wa Sh. 70 bilioni, kwa ajili ya kutatua shida ya maji katika kata ya Goba na maeneo ya jirani.
“Wilaya ya Ubungo tayari imeshatoa mkopo wa Tsh. Bilioni 2.6 kwa ajili ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Fedha hizi hazina riba hivyo tuchangamkie fursa hii kwa maendeleo yetu,” amesema Makori.
Makoro amewataka Wananchi wa kata hizo mbili na Wilaya kwa ujumla kujiandikisha kwenye orodha ya daftari la wapiga kura la Serikali za Mitaa.
“Nawasihi sana wananchi mkajiandikishe ili muweze kushiriki kwenye uchaguzi wa serikali za mitaa. Tukumbuke mwisho wa kujiandikisha ni Jumatatu ya tarehe 14 Oktoba, hivyo tumieni fursa hii ili muweze kuchagua viongozi wanaoeleweka na watakaotupatia maendeleo kwenye maeneo yetu.” amehimiza Makori.
Leave a comment