WIZARA ya Afya kupitia Baraza la Tiba asili na Tiba mbadala limeifungia dawa ya Hensha ambayo ni maarufu kwa jina la Mkongo yenye usajili namba TZ17TM0027 iliyokutwa imechanganywa na dawa ya kisasa ya nguvu za kiume inayoitwa Slidenafil. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Hayo yameelezwa leo tarehe 27 Julai, 2022 na Mwenyekiti wa Baraza hilo Prof. Hamisi Malebo wakati akitoa taarifa ya mwenendo wa utendaji wa Baraza hilo mbele ya Wajumbe wa Baraza hilo na Waandishi wa habari katika Mkoa wa Morogoro.
Amesema baraza hilo lilibaini hiyo ya mkongo imechanganywa na dawa ya kisasa ya nguvu za kiume inayoitwa Sildenafil kwa jina maarufu la biashara – Viagra ama Erecto kitendo ambacho ni kinyume na sheria na miongozo ya usajili wa dawa za tiba asili na mbadala.
Amesema baraza hilo kuanzia leo limefuta usajili wa dawa hiyo ya Hensha, inayomilikiwa na kituo cha Nyasosi Traditional Clinic.
Pia limekitaka kituo hicho kuhakikisha dawa hiyo inaondolewa sokoni mara moja kuanzia leo vinginevyo hatua kali ya kisheria itachukuliwa.
Amesisitiza kuwa baraza hilo litaendelea kufungia wote wanaofanya kazi kinyume na Sheria
Aidha, Prof. Malebo ameweka wazi kuwa, mganga ambaye anahitaji kutangaza dawa yake ni lazima afuate utaratibu wa kusajili dawa kwa kupima ubora na usalama na baadaye aombe kibali cha matangazo kutoka Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala.
Sambamba na hilo Prof. Malebo amesema, Baraza lilifanya uchunguzi na kubaini baadhi ya dawa kuwa na mapungufu madogo hasa kwenye uandishi wa lebo na vifungashio.
Amesema dawa mbili zilibainika kuwa na kiashiria cha hali duni ya usafi wa mazingira ya kutengenezea dawa hizo.
Vile vile, Prof. Malebo amesema, Baraza linaendelea kuwakumbusha wananchi kupata huduma kwa waganga na vituo ambavyo vimesajiliwa na Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala.
Pia amewataka kutumia dawa asili ambazo zimepimwa ubora na usalama pamoja na kusajiliwa na Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala.
Pia ametoa rai kuanza kuwasaka na kuwachukulia hatua za Kisheria Waganga wa tiba asili na tiba mbadala wanaotoa huduma kwa wananchi bila kisajiliwa na Baraza hilo kuanzia mwezi Februari 2023.
Leave a comment