SERIKALI imepiga marufuku wanafunzi wa kidato cha kwanza 2023 waliochaguliwa kujiunga na shule za kutwa, kuhamia shule za bweni, hadi zitakapotokea nafasi katika shule hizo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Marufuku hiyo imepigwa jana tarehe 29 Desemba 2022 na Katibu Mkuu, Wizara ya Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Prof. Riziki Shemdoe, katika kikao cha kufanya tathimini ya usimamizi na uendeshaji wa elimu nchini kwa 2022 kwa maafisa elimu wa mikoa.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na wizara hiyo, tangu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, Angellah Kairuki, atoe taarifa ya kuwapangia shule wanafunzi wa kidato cha kwanza kwa 2023, baadhi ya wazazi na walezi wametuma maombi ya kuwahamishia watoto wao kwenye shule za bweni.
Prof. Shemdoe alisema hakutakuwa na uhamisho huo kwa kuwa upangaji wanafunzi umefuata vigezo na taratibu zilizowekwa.
Alisema idadi ya wanafunzi waliopangiwa shule za bweni, imezingatia viwango vya juu vya ufaulu na nafasi zilizokuwepo katika shule hizo ili kuepusha msongamano kwa wanafunzi wa darasani na mahali pa kulala.
“OR-TAMISEMI inasisitiza kuwa hakuna uhamisho kutoka shule ya kutwa kwenda bweni kwasababu wale waliopangiwa bweni wamekidhi vigezo vya kuchaguliwa katika shule hizo.”
“Na kwa wanafunzi wenye changamoto za kimazingira, mfano amehama makazi ya awali wawasilishe changamoto hizo kwa Makatibu Tawala wa Mkoa ili zitatuliwe, maana upangaji wa wanafunzi kwenye shule umezingatia ukaribu wa shule na makazi ya wanafunzi hivyo endapo wamehama makazi ya awali kunaweza kutokea changamoto ya umbali,” alisema Prof. Shemdoe.
Hata hivyo, Prof. Shemdoe alisema endapo zitatokea nafasi za bweni zitakazohitajika kujazwa hapo baadae, maombi yatakayowasilishwa wizarani hapo yatachambuliwa na kamati maalum ambayo itaangalia sifa za walioomba kuhamishiwa huko.
Katika hatua nyingine, Prof. Shemdoe alitoa wito kwa wazazi kuhakikisha wanafunzi wote waliochaguliwa wanaripoti shuleni kwa wakati na kwamba hakutakuwa na chaguo la pili la mwanafunzi.
” Kwa mwaka huu hakutakuwa na chaguo la pili la wanafunzi kwasababu fedha zilizotolewa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan, katika sekta ya elimu zimetosha kuboresha miundombinu ya kuwachukua watoto wetu wote kwa intake(mkupuo) mmoja ,” alisema Prof. Shemdoe na kuongeza:
“Tangu Rais aingie madarakani ameshatoa fedha zilizowezesha kujenga zaidi ya vyumba vya madarasa 20,000 ndani ya miaka miwili hatua ambayo imewaondolea adha watoto kwa kuanza masomo kwa pamoja huku wazazi wakiwa hawajachangishwa kitu.”
Leave a comment