KUKAMILIKA kwa ujenzi wa jengo la Bohari ya Taifa ya chanjo, umesaidia kuokoa Sh. 10 bilioni kwa mwaka ambazo zingetumika katika kuhifadhi chanjo za watoto pamoja na vifaa. Anaripoti Hamisi Mguta …. (endelea).
Hayo yameelezwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alipofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa jengo hiyo lililogharimu Sh. 1.2 bilion akiongozana na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dk. Zainab Chaula.
Kwa kiasi kikubwa Waziri Ummy amesema ameridhishwa na hali ya ujenzi huo, hususan katika ujenzi wa vyumba vya kuhifadhia chanjo (stoo), jambo litalosaidia hasa wazazi wenye watoto wadogo kupata chanjo kwa wakati.
Pia, Waziri Ummy amempongeza Meneja Mpango wa Taifa wa chanjo Dk.Dafrosa Lyimo kwa kushirikiana na Mkandarasi kwa usimamizi mzuri wa jengo hilo hadi kufikia hatua ya mwisho.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Idara kuu ya Afya, Dk. Zainab Chaula ameahidi kuendelea kusimamia vizuri shughuli zote ili kuendelea kuboresha Sekta ya Afya kwa kasi ili wananchi wa hali zote wanufaike.
Kwa upande mwingine Dk. Zainab amesisitiza juu ya ushirikiano baina ya Watumishi katika Sekta ya Afya ili kurahisisha utendaji kazi kwa urahisi katika ngazi zote, hali itayosaidia wananchi kupata huduma bora.
Kwa upande wake Meneja Mpango wa Taifa wa Chanjo, Dk.Dafrosa Lyimo amesisitiza kwamba jengo hilo litakapokamilika litaleta faida nyingi katika kutoa huduma kwa wananchi ikiwemo kurahisisha usambazaji wa chanjo katika ngazi ya mkoa na kurahisisha upatikanaji wa chanjo hizo katika ngazi zote kwa wakati wowote.
Dk. Lyimo ameahidi kuendelea kusimamia kwa ukaribu shughuli zote za mpango huo ikiwemo upatikanaji wa Chanjo kwa wakati wote na mahali popote ili wananchi waendelee kupata huduma hiyo.
Leave a comment