KATIKA utekelezaji wa Mpango na Bajeti ya mwaka 2021/2022 Wizara ya Mambo, Serikali imelipatia jeshi la polisi helkopta moja kwaajili ya kutekeleza majukumu yake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yamebainishwa leo Alhamisi tarehe 5 Mei na Waziri Hamad Masauni wakati akiwasilisha bungeni makadiro ya mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2022/23.
Mbali na helkopta hiyo Masauni ametaja mafanikio mengine ya Wizara ni kununua magari 19 kwa ajili ya kusindikiza misafara ya Viongozi Wakuu wa Kitaifa; kununua magari 25 ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa ajili ya shughuli za utawala na ukaguzi na boti mbili za uokoaji.
Ametaja mafanikio mengine ni kukamilika kwa nyumba 119 za maafisa na askari wa Jeshi la Magereza katika maeneo mbalimbali nchini; kukamilika kwa ujenzi wa Ofisi ya Kamanda wa Polisi Singida; kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Zimamoto na Uokoaji Wilayani Chamwino – Dodoma; na ukamilishaji wa kituo cha Polisi Daraja C Mtambaswala – Mtwara.
“Mheshimiwa Spika, mafanikio mengine ni kukamilika kwa Kiwanda cha Maziwa katika Gereza Kingolwira – Morogoro, kukamilika kwa majengo ya kiwanda cha kuchakata na kupakia chumvi katika Gereza Lilungu – Mtwara, kukamilika kwa ujenzi wa Zahanati ya Polisi Wilaya ya Bariadi; kuanzishwa kwa Kambi ya Mafunzo ya Idara ya Uhamiaji katika eneo la Bomakichakamiba mkoani Tanga na kukamilisha ufungaji wa Mfumo wa Ki-elektroniki wa Usajili na Usimamizi wa Jumuiya (Registration of Societies Management Information System –RSMIS),” amesema Masauni.
Leave a comment