SERIKALI imesema licha ya malalamiko ya kuchelewa kwa ajira za walimu lakini hakuna wahitimu wa kutosha wa taaluma hiyo waliopeleka vyeti vyao ili waweze kupangiwa vituo vya kazi, anaandika Charles William.
Angela Kairuki, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora amesema kuwa serikali ilitangaza mchakato wa ajira za walimu wa masomo ya Sayansi na Hesabu ambapo kulikuwa na uhitaji wa walimu 8,000 (elfu nane) lakini ni walimu 2,100 (elfu mbili na mia moja) tu ndiyo waliopeleka vyeti vyao tayari kwa kuajiriwa.
“Sasa hivi tunajiuliza, je hao wengine waliokuwa wakiulizia ajira za serikali kila siku wako wapi mpaka sasa? Au ndiyo wenye vyeti feki? Nataka niwaambie kuwa hakuna mwenye cheti feki atakayeajiriwa wala kubakia kama mtumishi wa umma,” amesema Kairuki.
Kairuki ametoa taarifa hiyo wakati akizungumza na watumishi wa umma wanawake katika Manispaa ya Dodoma kwenye wiki ya maadhimisho ya miaka 40 ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
“Nitalisimamia kiukamilifu suala la watumishi na wahitimu walio na vyeti feki na ni bora niwe waziri anayechukiwa na jamii kuliko kulifumbia macho suala la vyeti feki,” amesema.
Hata hivyo, Kairuki hakuweza kueleza hatima ya ajira za walimu wa masomo ya sanaa ikizingatiwa ni zaidi ya miaka miwili sasa tangu serikali ilipoajiri walimu hao kwa mara ya mwisho.
Katika hatua nyingine Kairuki ametangaza kuwa ifikapo Machi mwaka huu watumishi wote wa umma ambao hawajawasilisha vyeti vyao halisi vya kitaaluma watafukuzwa kazi.
“Tumetoa muda wa kutosha kwa watumishi wa umma kuwasilisha vyeti vyao vya kitaaluma, lakini jambo la kusikitisha ni kwamba mpaka sasa kuna baadhi ya watumishi bado hawajawasilisha vyeti au hata namba ya utambulisho (index number).
“Tutawafukuza kazi bila kumuonea mtu huruma. Serikali ya sasa haitaki mchezo, lazima kila mtumishi alipwe mshahara kulingana na taaluma na kazi anayoifanya,” amesema.
Leave a comment