KATIKA kuimarisha usimamizi wa miradi ya kupeleka umeme vijini, Serikali imesema inakwenda kuajiri waratibu wa miradi ya umeme vijijini kwa kila jimbo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Hayo yamebainishwa leo Jumatano tarehe 1 Juni, 2022 na Waziri wa Nishati, Januari Makamba, akiwasilisha bajeti yam waka 2022/2023.
Mbali na kuimarisha usimamizi wa miradi Makamba amesema pia Waratibu watarahisisha upatikani wa taarifa za maendeleo ya miradi hiyo.
“Waratibu hao watakuwa kiungo cha mawasiliano na taarifa kati ya Wabunge, viongozi wa kisiasa, wakandarasi, REA na wadau wengine,” amesema Makamba.
Ameongeza kwa kushirikiana na TANESCO, waratibu hao watakuwa na wajibu wa kutoa taarifa za mara kwa mara kwa viongozi ikiwemo wa Wabunge kuhusu maendeleo ya miradi.
Katika hatua nyingine Makamba amesema Serikali imesikia kilio cha muda mrefu cha wananchi wanaoishi katika maeneo ya mijini yenye sifa zinazolingana na vijiji huku wakilipa bei ya kuunganishiwa umeme ya mijini.
“Nataka niwahakikishie kwamba tumesikia kilio chao na tayari tumeunda timu inayojumuisha Wizara ya Nishati, TANESCO na REA.
“Timu hii itazunguka katika miji yote na kuyabaini maeneo hayo kwa kuwashirikisha Waheshimiwa Wabunge wa maeneo husika.
Amesema maeneo yatakayobainishwa na timu hiyo yatajumuishwa kwenye bei ya vijiji yaani Sh. 27,000, “zoezi hili litafanyika nchi nzima na kukamilishwa ndani ya miezi sita.”
Leave a comment