WAZIRI wa Nishati, January Makamba, amesema wizara yake imeandaa waraka wa uanzishwaji kanuni zitakazowezesha uundwaji wa hifadhi ya kimkakati ya kitaifa ya mafuta, ili kukabiliana na changamoto ya kupanda kwa bei ya bidhaa hiyo katika soko la dunia. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Makamba ametoa taarifa hiyo leo Jumanne, tarehe 6 Aprili 2022, jijini Dar es Salaam, akitoa ufafanuzi kuhusu changamoto ya mfumuko wa bei ya mafuta nchini.
Waziri huyo wa nishati amesema mabadiliko hayo ya kanuni yatapelekwa katika Bunge la Bajeti.
“Kumekuwa na kamati mbalimbali za kushughulikia suala la mafuta, ambayo kumekuwa na mapendekezo mbalimbali ya kuboresha na kuimarisha tasnia hii na bahati nzuri sisi tunafanyia kazi na kwenye Bunge la Bajeti tutatoa taarifa na muelekeo wa mambo mapya makubwa,” amesema Makamba.
Makamba amesema “ikiwemo jambo ambalo kwa muda mrefu tumekuwa tunalitaka la hifadhi ya kimakakati ya taifa ya mafuta. Tumeandaa waraka ambao tutupeleka mbele kwa ajili ya uwezeshaji pamoja na kanuni mpya ya uanzishwa hifadhi hiyo, tuwe na uwezo wa kuhimili mabadiliko hayo.”
Amesema bei ya mafuta katika soko la dunia imepanda maradufu, ambapo bei ya petroli imepanda kutoka Dola za Marekani 561 kwa tani moja (2021), hadi kufikia dola 911, wakati dizeli bei yake ikipanda kutoka dola 503 hadi 823, katika kipindi hiko.
Makamba amesema kupanda kwa bei ya mafuta kulianza kusababishwa na janga la Ugonjwa wa Virusi vya Korona (UVIKO-19), ulioibuka mwishoni mwa 2019, kisha ikachochewa zaidi ya mgogoro wa kivita kati ya Urusi na Ukraine.
Leave a comment