SERIKALI ya Jamhuri imeeleza kuwa, imefungua mlango wa majadiliano kuhusu kubadili Sheria ya Vyombo vya Habari ya Mwaka 2016. Anaripoti Faki Sosi … (Endelea).
Kauli hiyo imetolewa baada ya serikali kukutana na Taasisi ya Habari ya Kimataifa (IPI) na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) jijini Dodoma terehe 2 Aprili mwaka huu.
Leo terehe 4 Aprili Mwaka 2019, viongozi wa TEF na IPI wamekutana na waandishi wa habari kuwaeleza nia ya ziara ya IPI, kusaidia wanahabari na vyombo vya habari nchini kukua na kufikia kiwango cha kimataifa.
Akitoa ufafanuzi Deudatus Balile, Kaimu Mwenyekiti wa TEF amesema kuwa, ziara hiyo imefenywa na IPI baada ya kusikia, Tanzania kuna changamoto za wanahabari na vyombo vya habari.
Balile amesema, IPI na TEF walikutana na Harrison Mwakyembe, Waziri wa Habari Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye alisema, yuko tayari kushirikiana na wadau kurekebisha Sheria ya Vyombo vya Habari (2016) inayolalamikiwa.
“Dk. Mwakyembe alikubaliana na ujumbe huo juu ya nia ya kushirikisha wadau wa habari kufikia malengo ya pamoja ambayo ni kuboresha taaluma ya habari Tanzania.”
Balile amesema, ujumbe huo ulikaa meza ya mazungumzo na Spika wa Bunge, Job Ndugai na wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
“Viongozi hao wamesisitiza uandishi wenye viwango na uhuru wa vyombo vya habari kuwa ni muhimu katika kufanikisha ajenda za maendeleo za kitaifa ikiwamo mapambano dhidi ya rushwa,” amesema Balile.
Amesema, IPI kwa kushirikiana na wenyeji wao TEF, wamekuja Tanzania kuanzisha mazungumzo juu ya masuala yanayoathiri vyombo vya habari na uhuru wa habari.
Ujumbe wa IPI umeongozwa na Makamu Mwenyekiti, Khadija Patel ambaye ni Mhariri Mkuu wa Gazeti la Mail & Guardian la nchini Afrika Kusini.
Ameambatana na Carsten von Nahmen, mwanachama wa IPI na Mkuu wa Idara ya Mafunzo ya Deutsche Welle (DW) Akademie ya Ujerumani; Naibu Mkurugenzi wa IPI, Scott Griffen na Mkurugenzi wa Uzengezi wa IPI Ravi R. Prasad.
IPI ni mtandao wa wahariri kimataifa, viongozi wa vyombo vya habari, wamiliki na waandishi waandamizi ambapo jukumu lao kubwa ni kuimarisha huru wa vyombo vya habari na kuboresha taaluma ya uandishi wa habari.
Makamu Mwenyekiti wa IPP, Khadija amesema, wamefurahishwa na nia ya serikali kushirikiana na wadau wa habari kwa uwazi kubadili sheria za habari nchini, kuboresha ubora na uhuru wa vyombo vya habari kwa njia ya mazungumzo.
Wiki iliyopita, Mahakama ya Afrika Mashariki ilitoa hukumu kuwa, baadhi ya vifungu vya sheria hiyo iliyotungwa mwaka 2016, vinazuia uhuru wa kujieleza na vinakinzana na Mkataba wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Leave a comment