SERIKALI imeeleza kwamba, pindi taratibu zitakapokamilika, wachimbaji katika Wilaya ya Mbogwe, Geita watapatiwa leseni za uchimbaji. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa kufuatiwa swali la Augustino Masele amelohoji je, serikali itatoa leseni za kuchimba dhahabu kwa vikundi vya wachimbaji wilayani Mbogwe?
Aliongeza, Wilaya ya Mbogwe ina madini ya dhahabu katika maeneo mbalimbali na kuna vikundi vya wachimbaji vimeundwa ili kuchimba dhahabu.
Katika majibu yake, Wizara ya Madini leo tarehe 18 Mei 2020 imeeleza, katika Wilaya ya Mbogwe, Geita maeneo mawili yenye ukubwa wa hekta 547.87 yametengwa kwa ajili ya uchimbaji mdogo wa madini.
“Vikundi viwili vya wigunanhi Group na Hekima Group vimepatiwa leseni, vikundi vingine viwili vya Isanjabadungu na Numbagintale Gold Mining Cooperate Union vimewasilisha maombi ya leseni za uchimbaji katika maeneo hayo na watapatiwa leseni pindi taratibu za kisheria zitakapokamilika hivi karibuni,” imeeleza wizara hiyo.
Wizara imeeleza, serikali kupitia Wizara ya Madini imekuwa ikitenga maeneo maalumu kwa ajili ya uchimbaji mdogo wa madini, ambapo jumla ya maeneo 46 katika sehemu mbalimbali nchini yenye ukubwa wa hekta 281,533.69 yametengwa.
Na kwamba, katika wilaya hiyo ya Mbogwe, maeneo mengine nchini kwa ujumla yataendelea kutengwa kama ilivyoainishwa katika kifungu cha 16 cha Sheria ya Madini ya Mwaka 2010 Sura ya 123.
“Wizara kwa kutumia taasisi zake za GST na STAMICO, itaendelea kufanya utafiti ili kubaini uwepo wa mashapo ya madini katika maeneo mbalimbali nchini, na kuyatenga kwa ajili ya uchimbaji mdogo wa madini. Hii itawezesha wachimbaji wadogo wa madini kufanya uchimbaji wa madini wenye tija,” wizara imeeleza katika majibu yake.
Leave a comment