Serikali ya Tanzania imewaita mezani viongozi wa Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS), kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha mahusiano ya pande zote mbili. Anaripoti Hamis Mguta, Arusha … (endelea).
Wito huo umetolewa leo Alhamisi tarehe 14 Aprili 2021, na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Amon Mpanju wakati akifungua Mkutano Mkuu wa TLS unaofanyika jijini Arusha.
Mpanju ameutaka uongozi mpya wa TLS utakaochaguliwa kesho Ijuma tarehe 16 Aprili 2021, kukaa meza moja na Serikali kujadili changamoto zilizopo ikiwepo baadhi ya vifungu vya sheria vinavyodaiwa kuwa kandamizi kwa tasnia hiyo.
“Niombe uongozi unaokuja tuwe na nia njema, tutizame mabadiliko ya sheria yaliyopo kama yataleta ufanisi na kama haitaketa ufanisi serikali iko tutakaa mezani tuangalie. Lakini tusianze kupinga mwanzo.
“Ni wakati uongozi mpya kukaa kutengeneza hoja na kwenda mezani. Haileti tija kusimama hapa kutoa tamko bila kushauriana na wanaohusika sote tuanjenga nyumba moja,” amesema Mpanju.
Mpanju ametoa kauli hiyo baada ya Rais wa TLS anayemaliza muda wake, Dk. Lugemeleza Nshala, kusema mabadiliko ya Sheria inayoongoza chama hicho, yaliyofanyika mwaka jana, yanababa uhuru wa chama hicho na mawakili kutekeleza majukumu yao.
Sambamba na hilo, Mpanju amewaasa viongozi wa TLS kutojihusisha na masuala ya siasa na uanaharakati.
“Haina masilahi wala tija kujiingiza kwenye uanaharakati na kuacha jukumu la msingi la kitaaluma. Haina haja wa tija kujiingiza kwenye siasa. Nawasihi viongozi watakaokuja nenda kwenye msingi wa malengo ya serikali ya kukuza chama na taaluma ya Sheria,” amesema Mpanju.
Leave a comment