WAZIRI wa Maliasili na Utalii, Balozi Dk. Pindi Chana amesema vikosi vya ulinzi na usalama kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wanaoendelea na kazi ya kuzima moto wamefanikiwa kuudhibiti moto huo katika maeneo mengi ya mlima Kilimanjaro.
Aidha, amesema moto huo uliokuwa unawaka kutoka katika Kituo cha Millenium kuelekea Marangu Hut na Mweka Hut nao umedhibitiwa kabla ya kufika katika vituo hivyo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Katika taarifa aliyoitoa kwa umma leo tarehe 23 Oktoba 2022, amesema tarehe 21 Oktoba, 2022 muda wa saa 2.30 usiku baadhi ya maeneo ya Hifadhi yetu ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro yaliwaka moto uliokuwa ukitokea eneo la Karanga kuelekea Baranco.
Amesema juhudi za kuuzima moto huo zilianza mara moja zikihusisha vyombo vya ulinzi na usalama, taasisi mbalimbali za wizara ya Maliasili na Utalii, wadau wa utalii na uhifadhi kutoka makampuni mbalimbali ya Utalii hapa nchini na wananchi.
“Kufuatia juhudi hizi, napenda kuutangazia umma kuwa vikosi vinavyoendelea na kazi ya kuzima moto vimefanikiwa kuudhibiti moto huo katika maeneo mengi ya mlima huo.
“Juhudi zaidi zimeelekezwa katika eneo lenye korongo kubwa la Karanga ambapo vikosi vinavyoendelea na kazi ya kuzima moto viko katika eneo hilo kuhakikisha moto huo pia unadhibitiwa,” amesema.
Amesema kwa ujumla zoezi linaendelea vizuri na tuna matumaini ya kuudhibiti moto huo kadri muda unavyokwenda.
“Natoa shukrani za dhati kwa ushirikiano mkubwa tuliopata kutoka kwa vyombo vya ulinzi na usalama, taasisi mbalimbali za wizara ya Maliasili na Utalii, wadau wa utalii na uhifadhi, wanahabari, mashirika mbalimbali na wananchi kwa kujitoa kwa hali na mali katika jukumu hili la kuhakikisha Mlima Kilimanjaro unakuwa salama na shughuli za utalii zinaendelela kama kawaida,” amesema.
Leave a comment