MSEMAJI wa Serikali, Dk. Hassan Abbas amesema kutokana na maoni mbalimbali serikali imeridhia mashabiki watakaotaka kwenda viwanjani kutazama mechi mara tu baada ya ligi kuanza waruhusiwe kuwepo kwa kuzingatia muongozo wa Wizara ya Afya. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Dk. Abbas ambaye pia ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ameyasea hayo leo tarehe 31 Mei 2020 alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu maagizo ya serikali kufuatia kuruhusiwa kwa michezo nchini.
Amesema wadau wote wa michezo wanapaswa kuusoma muongozo wa wizara ya afya kuhusu tahadhari za kuchukua wakati wa ligi kuendelea ili kujikinga na maambukizi ya virusi vya Corona (Covid-19).
Amesema kwa yeyote atakaye kiuka muongozo huo hatua zitachukuliwa kulingana na kiwango cha kukiuka muongozi huo.
Hata hivyo Dk. Abbas amesema licha ya mashabiki kuruhusiwa kuingia kushuhudia mechi hizo, zipo baadhi ya mechi kubwa zinazotazamiwa kuwa na mashabiki wengi hivyo ni nusu ya idadi ya mashabiki wanaopaswa kuingia uwanjani tu ndio watakaopata nafasi ya kuingia uwanjani ili kupunguza msongamano.
“Tumeruhusu mashabiki wawepo viwanjani lakini zitaangaliwa baadhi ya mechi, mechi kama ni kubwa maelekezo ni kwamba wataingia nusu ya mashabiki wanaotakiwa kuingia,” amesema Dk. Abbas.
Aidha, hatuka hatua nyingine Dk. Abbas amesema awali kulikuwa na maoni ya kwamba ligi ichezwe kituo kimoja lakini wadau wamekuwa na maoni tofauti hivyo serikali imeridhia ligi ichezwe kwa mtindo wa ugenini.
“Serikali imeruhusu mechi za ligi za soka zichezwe kwa mfumo kama ilivyokuwa kabla ya Covid 19 kwa muhtadha huo mechi zitachezwa nyumbani na ugenini hakutakuwa na habari ya vituo,” amesema.
Serikali ilitoa agizo la kusimamishwa kwa shughuli za michezo yote pamoja na shule Machi 17 2020 ili kupunguza maambukizi ya ugonjwa wa Covid-19 na sasa baadhi ya shughuli zimeanza kuruhusiwa ikiwemo michezo na vyuo kutokana na kile kinachoelezwa kuwa maambukizi ya ugonjwa huo yamepungua nchini.
Leave a comment