HATIMAYE mazungumzo kati ya Tanzania na Kampuni ya Barrick Gold kuhusu sekta ya madini yaliyodumu kwa takribani miezi mitano yamehimitishwa jijini Dar es Salaam, anaandika Faki Sosi.
Rais John Magufuli leo amepokea ripoti ya makubaliano hayo ambayo yalihusisha watalaam 25 kutoka kampuni ya Barrick na wawakilishi wanane wa Tanzania wakiongozwa na Waziri wa Katiba na Sheria Profesa Palamagamba Kabudi.
Moja ya makubaliano yaliyofikiwa ni pamoja na Tanzania kugawana faida 50 kwa 50 na kampuni ya Barrick Gold .
Aidha, katika makubaliano hayo Barrick wamekubali kulipa fedha mbalimbali kwa Halmashauri wanapochimba dhahabu.
Kupitia makubaliano hayo, kampuni hiyo imekubali kupanua wigo wa ajira kwa Watanzania pamoja na kujenga maabara na kiwanda cha kuchakata makanikia hapa nchini.
Profesa Kabudi amesema kampuni ya Barrick, wamekubali masharti yote yaliyoko kwenye sheria mpya ya madini na kukubali kuingia ubia wa asilimia 50 kwa 50 kwenye biashara ya madini.
Kwa upande wake, mwenyekiti mtendaji wa kampuni ya Barrick Gold Profesa . John Thornton alimpongeza Rais Magufuli kwa uamuzi wa kutaka muafaka juu ya makanikia.
“Tumekubaliana kulipa dola za Marekani milioni 300 sawa na Sh. bilioni 700 kama sehemu ya kujenga uaminifu na kuendeleza biashara,” amesema
Rais Magufili amesema baada ya kukamilika mazungumzo haya sasa watalaam wa Tanzania waanze kujadiliana katika sekta ya Almasi na Tanzanite.
Leave a comment